Mithali 15:1-33 ONEN
[1] Jawabu la upole hugeuza ghadhabu, bali neno liumizalo huchochea hasira. [2] Ulimi wa mwenye hekima husifu maarifa, bali kinywa cha mpumbavu hufoka upumbavu. [3] Macho ya BWANA yako kila mahali, yakiwaangalia waovu na wema. [4] Ulimi uletao uponyaji ni mti wa uzima, bali ulimi udanganyao huponda roho. [5] Mpumbavu hubeza maonyo ya baba yake, bali yeyote akubaliye maonyo huonyesha busara. [6] Nyumba ya mwenye haki ina hazina kubwa, bali mapato ya waovu huwaletea taabu. [7] Midomo ya mwenye hekima hueneza maarifa, bali sivyo ilivyo mioyo ya wapumbavu. [8] BWANA huchukia sana dhabihu za waovu, bali maombi ya wanyofu humfurahisha Mungu. [9] BWANA huchukia sana njia ya waovu, bali huwapenda wale wafuatao haki. [10] Adhabu kali humngoja yeye aachaye njia; yeye achukiaye maonyo atakufa. [11] Mauti na Uharibifu viko wazi mbele za BWANA: je, si zaidi sana mioyo ya wanadamu! [12] Mwenye mzaha huchukia maonyo; hatataka shauri kwa mwenye hekima. [13] Moyo wenye furaha hufanya uso uchangamke, bali maumivu ya moyoni huponda roho. [14] Moyo wa mwenye ufahamu hutafuta maarifa, bali kinywa cha mpumbavu hujilisha upumbavu. [15] Siku zote za wanaoonewa ni za taabu, bali moyo mchangamfu una karamu ya kudumu. [16] Afadhali kuwa na kidogo pamoja na kumcha BWANA, kuliko mali nyingi pamoja na ghasia. [17] Afadhali chakula cha mboga mahali palipo na upendo kuliko nyama ya ndama iliyonona pamoja na chuki. [18] Mtu mwepesi wa hasira huchochea ugomvi, bali mtu mvumilivu hutuliza ugomvi. [19] Njia ya mvivu imezibwa na miiba, bali njia ya mwenye haki ni barabara kuu. [20] Mwana mwenye hekima huleta furaha kwa baba yake, bali mtu mpumbavu humdharau mama yake. [21] Upumbavu humfurahisha mtu ambaye hana akili, bali mtu mwenye ufahamu hushika njia iliyonyooka. [22] Mipango hushindwa kufanikiwa kwa ajili ya kukosa ushauri, bali kukiwa na washauri wengi hufanikiwa. [23] Mtu hupata furaha katika kutoa jibu linalofaa: je, ni zuri namna gani neno lililotoka kwa wakati wake! [24] Mapito ya uzima huelekea juu kwa ajili ya wenye hekima kumwepusha asiende chini kaburini. [25] BWANA hubomoa nyumba ya mtu mwenye kiburi, bali huilinda mipaka ya mjane isiguswe. [26] BWANA huchukia sana mawazo ya mwovu, bali mawazo ya wale walio safi humfurahisha yeye. [27] Mtu mwenye tamaa huletea jamaa yake taabu, bali yeye achukiaye rushwa ataishi. [28] Moyo wa mwenye haki hupima majibu yake, bali kinywa cha mwovu hufoka ubaya. [29] BWANA yuko mbali na waovu, bali husikia maombi ya wenye haki. [30] Mtazamo wa tabasamu huleta furaha moyoni, nazo habari njema huipa mifupa afya. [31] Yeye asikilizaye maonyo yatoayo uzima atakuwa miongoni mwa wenye hekima. [32] Yeye anayedharau maonyo hujidharau mwenyewe, bali yeyote anayekubali maonyo hupata ufahamu. [33] Kumcha BWANA humfundisha mtu hekima, nao unyenyekevu huja kabla ya heshima.
