Mithali 14:1-35 ONEN
[1] Mwanamke mwenye hekima huijenga nyumba yake, bali mpumbavu huibomoa nyumba yake kwa mikono yake mwenyewe. [2] Yeye ambaye njia zake ni nyofu humcha BWANA, bali yeye ambaye njia zake zimepotoka humdharau Mungu. [3] Mazungumzo ya mpumbavu huleta fimbo mgongoni mwake, bali mwenye hekima hulindwa na maneno ya midomo yake. [4] Pale ambapo hakuna mafahali, hori ni tupu, bali kutokana na nguvu za fahali huja mavuno mengi. [5] Shahidi mwaminifu hadanganyi, bali shahidi wa uongo humimina uongo. [6] Mwenye mzaha huitafuta hekima na haipati, bali maarifa huja kwa urahisi kwa anayepambanua. [7] Kaa mbali na mtu mpumbavu, kwa maana hutapata maarifa katika midomo yake. [8] Hekima ya mwenye busara ni kufikiria njia zake, bali upumbavu wa wapumbavu ni udanganyifu. [9] Wapumbavu hudhihaki kujirekebisha kutoka dhambi, bali wema hupatikana miongoni mwa wanyofu. [10] Kila moyo hujua uchungu wake wenyewe, wala hakuna yeyote awezaye kushiriki furaha yake. [11] Nyumba ya mwovu itaangamizwa, bali hema la mnyofu litastawi. [12] Iko njia ionekanayo kuwa sawa kwa mtu, bali mwisho wake huelekeza mautini. [13] Hata katika kicheko moyo waweza kuuma, nayo furaha yaweza kuishia katika majonzi. [14] Wasio na imani watapatilizwa kikamilifu kwa ajili ya njia zao, naye mtu mwema atapewa thawabu kwa ajili ya njia yake. [15] Mtu mjinga huamini kila kitu, bali mwenye busara hufikiria hatua zake. [16] Mtu mwenye hekima humcha BWANA na kuepuka mabaya, bali mpumbavu hukasirika kwa hamaki na uzembe. [17] Mtu anayekasirika kwa haraka hufanya mambo ya upumbavu, naye mtu wa hila huchukiwa. [18] Mjinga hurithi upumbavu, bali wenye busara huvikwa maarifa kichwani kama taji. [19] Watu wabaya watasujudu mbele ya watu wema, nao waovu kwenye malango ya wenye haki. [20] Maskini huepukwa hata na majirani zao, bali matajiri wana marafiki wengi. [21] Yeye anayemdharau jirani yake hutenda dhambi, bali amebarikiwa yeye aliye na huruma kwa mhitaji. [22] Je, wale wanaopanga ubaya hawapotoki? Bali wale wanaopanga kilicho chema hupata upendo na uaminifu. [23] Kazi zote zinazofanywa kwa bidii huleta faida, bali mazungumzo matupu huelekea umaskini tu. [24] Utajiri wa wenye hekima ni taji yao, bali upumbavu wa wapumbavu huzaa upumbavu. [25] Shahidi wa kweli huokoa maisha, bali shahidi wa uongo ni mdanganyifu. [26] Yeye amchaye BWANA ana ngome salama, na kwa watoto wake itakuwa kimbilio. [27] Kumcha BWANA ni chemchemi ya uzima, ili kumwepusha mtu na mitego ya mauti. [28] Wingi wa watu ni utukufu wa mfalme, bali pasipo watu mkuu huangamia. [29] Mtu mwenye subira ana ufahamu mwingi, bali anayekasirika haraka huonyesha upumbavu. [30] Moyo wenye amani huupa mwili uzima, bali wivu huozesha mifupa. [31] Yeye amwoneaye maskini huonyesha dharau kwa Muumba wao, bali yeyote anayemhurumia mhitaji humheshimu Mungu. [32] Waovu huangamizwa kwa matendo yao maovu, bali hata katika kifo wenye haki hupata kimbilio. [33] Hekima hukaa katika moyo wa mwenye ufahamu bali haijulikani miongoni mwa wapumbavu. [34] Haki huinua taifa, bali dhambi ni aibu kwa watu wote. [35] Mfalme hupendezwa na mtumishi mwenye hekima, bali ghadhabu yake humwangukia mtumishi mwenye kuaibisha.
