[1] Mwana mwenye hekima husikia mafundisho ya babaye, bali mwenye dharau hasikilizi maonyo. [2] Kutoka tunda la midomo yake mtu hufurahia mambo mema, bali wasio waaminifu wanatamani sana jeuri. [3] Yeye alindaye midomo yake hulinda nafsi yake, bali yeye asemaye kwa haraka ataangamia. [4] Mvivu hutamani sana na hapati kitu, bali nafsi ya mwenye bidii hutoshelezwa kikamilifu. [5] Mwenye haki huchukia uongo, bali waovu huleta aibu na fedheha. [6] Haki humlinda mtu mwadilifu, bali uovu humwangusha mwenye dhambi. [7] Mtu mmoja hujifanya tajiri, kumbe hana chochote; mwingine hujifanya maskini, kumbe ana utajiri mwingi. [8] Utajiri wa mtu waweza kukomboa maisha yake, bali mtu maskini hasikii kitisho. [9] Nuru ya mwenye haki hungʼaa sana, bali taa ya mwovu itazimwa. [10] Kiburi huzalisha magomvi tu, bali hekima hupatikana kwa wale wanaozingatia ushauri. [11] Fedha isiyo ya halali hupungua, bali yeye akusanyaye fedha kidogo kidogo huongezeka. [12] Kilichotarajiwa kikikawia kuja moyo huugua, bali tumaini lililotimizwa ni mti wa uzima. [13] Yeye anayedharau mafundisho anajiletea maangamizi, bali yeye anayeheshimu agizo hupewa tuzo. [14] Mafundisho ya mwenye busara ni chemchemi ya uzima, ili kumwepusha mtu na mitego ya mauti. [15] Ufahamu mzuri hupata upendeleo, bali njia ya asiye mwaminifu ni ngumu. [16] Kila mwenye busara hutenda kwa maarifa, bali mpumbavu hudhihirisha upumbavu wake. [17] Mjumbe mwovu huanguka kwenye taabu, bali mjumbe mwaminifu huleta uponyaji. [18] Yeye anayedharau maonyo hupata umaskini na aibu, bali yeye anayekubali maonyo huheshimiwa. [19] Tarajio lililotimizwa ni tamu kwa nafsi, bali wapumbavu huchukia sana kuacha ubaya. [20] Yeye atembeaye na mwenye hekima atapata hekima, bali rafiki wa mpumbavu hupata madhara. [21] Balaa humwandama mtenda dhambi, bali mafanikio ni thawabu kwa mwenye haki. [22] Mtu mwema huwaachia wana wa wanawe urithi, bali mali ya wenye dhambi imehifadhiwa kwa ajili ya wenye haki. [23] Shamba la mtu maskini laweza kuzalisha chakula kingi, bali dhuluma hukifutilia mbali. [24] Yeye aizuiaye fimbo yake hampendi mwanawe, bali yeye ampendaye huwa mwangalifu kumwadibisha. [25] Mwenye haki hula mpaka akaridhisha moyo wake, bali tumbo la mwovu hutaabika kwa njaa.