Mithali 12:1-28 ONEN
[1] Yeyote apendaye kuadibishwa hupenda maarifa, bali yeye achukiaye kuonywa ni mpumbavu. [2] Mtu mwema hupata kibali kutoka kwa BWANA, bali BWANA humhukumu mwenye hila. [3] Mtu hathibitiki kutokana na uovu, bali mwenye haki hataondolewa. [4] Mke mwenye tabia nzuri ni taji ya mumewe, bali aaibishaye ni kama uozo katika mifupa ya mumewe. [5] Mipango ya mtu mwadilifu ni ya haki, bali ushauri wa mwovu ni udanganyifu. [6] Maneno ya waovu huotea kumwaga damu, bali maneno ya waadilifu huwaokoa. [7] Watu waovu huondolewa na kutoweka, bali nyumba ya mwenye haki husimama imara. [8] Mtu husifiwa kulingana na hekima yake, bali watu wenye akili zilizopotoka hudharauliwa. [9] Heri mtu wa hali ya chini mwenye mtumishi, kuliko kujifanya mtu wa hali ya juu nawe huna chakula. [10] Mtu mwenye haki hujali mahitaji ya mnyama wake, bali matendo ya huruma ya mwovu ni ukatili. [11] Yeye alimaye shamba lake atakuwa na chakula tele, bali yeye afuataye mambo ya upuzi hana akili. [12] Waovu hutamani mateka ya watu wabaya, bali shina la mwenye haki hustawi. [13] Mtu mwovu hunaswa kwa mazungumzo yake ya dhambi, bali mwenye haki huepuka taabu. [14] Kutokana na tunda la midomo yake mtu hujazwa na mambo mema, hakika kama ilivyo kazi ya mikono yake humtunza. [15] Njia ya mpumbavu huonekana sawa machoni pake mwenyewe, bali mtu mwenye hekima husikiliza ushauri. [16] Mpumbavu huonyesha kuudhika kwake mara moja, bali mtu wa busara hupuuza matukano. [17] Shahidi wa kweli hutoa ushuhuda wa kuaminika, bali shahidi wa uongo husema uongo. [18] Maneno ya kipumbavu huchoma kama upanga, bali ulimi wa mwenye hekima huleta uponyaji. [19] Midomo isemayo kweli hudumu milele, bali ulimi wa uongo hudumu kwa muda mfupi tu. [20] Upo udanganyifu katika mioyo ya wale ambao hupanga mabaya, bali kuna furaha kwa wale wanaoleta amani. [21] Hakuna dhara linalompata mwenye haki, bali waovu wana taabu nyingi. [22] BWANA anachukia sana midomo idanganyayo, bali hufurahia watu ambao ni wa kweli. [23] Mtu mwenye busara hujihifadhia maarifa yeye mwenyewe, bali moyo wa wapumbavu hububujika upumbavu. [24] Mikono yenye bidii itatawala, bali uvivu huishia katika kazi za utumwa. [25] Moyo wa wasiwasi humlemea mtu, bali neno la huruma humfurahisha. [26] Mtu mwenye haki ni mwangalifu katika urafiki, bali njia ya waovu huwapotosha. [27] Mtu mvivu haoki mawindo yake, bali mtu mwenye bidii ana mali za thamani. [28] Katika njia ya haki kuna uzima; katika mapito hayo kuna maisha ya milele.
