Mithali 11:1-31 ONEN
[1] BWANA huchukia sana mizani za udanganyifu, bali vipimo sahihi ni furaha yake. [2] Kiburi kinapokuja, ndipo huja aibu, bali unyenyekevu huja na hekima. [3] Uadilifu wa wenye haki huwaongoza, bali wasio waaminifu huharibiwa na hila yao. [4] Utajiri haufaidi kitu katika siku ya ghadhabu, bali haki huokoa kutoka mautini. [5] Haki ya wasio na lawama, huwatengenezea njia iliyonyooka, bali waovu huangushwa kwa uovu wao wenyewe. [6] Haki ya wanyofu huwaokoa, bali wasio waaminifu hunaswa na tamaa mbaya. [7] Wakati mtu mwovu anapokufa, matumaini yake hutoweka; yote aliyoyatazamia kutokana na nguvu zake huwa si kitu. [8] Mtu mwenye haki huokolewa kutoka taabu, naye mtu mwovu huingia humo badala yake. [9] Kwa kinywa chake mtu asiyemwamini Mungu humwangamiza jirani yake, bali kwa maarifa mwenye haki huokolewa. [10] Wakati mwenye haki anapofanikiwa, mji hufurahi; mwovu atowekapo, kuna kelele za furaha. [11] Kutokana na baraka ya mtu mnyofu mji hukwezwa, bali kwa kinywa cha mwovu mji huharibiwa. [12] Mtu asiye na akili humdharau jirani yake, bali mtu mwenye ufahamu huuzuia ulimi wake. [13] Masengenyo husaliti tumaini, bali mtu mwaminifu hutunza siri. [14] Pasipo ushauri wa hekima taifa huanguka, bali washauri wengi hufanya ushindi uwe wa hakika. [15] Yeye amdhaminiye mgeni hakika atateseka, bali yeyote akataaye kuunga mkono dhamana ni salama. [16] Mwanamke mwenye moyo wa huruma hupata heshima, bali wanaume wakorofi hupata mali tu. [17] Mwenye huruma hujinufaisha mwenyewe, bali mkatili hujiletea taabu mwenyewe. [18] Mtu mwovu hupata ujira wa udanganyifu, bali yeye apandaye haki huvuna tuzo ya uhakika. [19] Mtu mwenye haki kweli kweli hupata uzima, bali yeye afuatiliaye ubaya huendea kifo chake. [20] BWANA huwachukia sana watu wenye moyo wa upotovu, bali hupendezwa na wale ambao njia zao hazina lawama. [21] Uwe na hakika na hili: Waovu hawataepuka kuadhibiwa, bali wenye haki watakuwa huru. [22] Kama pete ya dhahabu katika pua ya nguruwe ndivyo alivyo mwanamke mzuri ambaye hana busara. [23] Shauku ya mwenye haki huishia tu kwenye mema, bali tumaini la mwovu huishia tu kwenye ghadhabu. [24] Kuna mtu atoaye kwa ukarimu, hata hivyo hupata zaidi, mwingine huzuia, lakini huwa maskini. [25] Mtu mkarimu atastawi; yeye awaburudishaye wengine ataburudishwa mwenyewe. [26] Watu humlaani mtu awanyimae watu nafaka, bali baraka itamkalia kichwani kama taji yeye aliye radhi kuiuza. [27] Yeye atafutaye mema hupata ukarimu, bali ubaya huja kwake yeye autafutaye. [28] Yeyote ategemeaye utajiri wake ataanguka, bali mwenye haki atastawi kama jani bichi. [29] Yeye aletaye taabu kwa jamaa yake atarithi tu upepo, naye mpumbavu atakuwa mtumishi wa wenye hekima. [30] Tunda la mwenye haki ni mti wa uzima, naye mwenye hekima huvuta roho za watu. [31] Kama wenye haki watapokea ujira wao duniani, si zaidi sana yule asiyemcha Mungu na mwenye dhambi?
