Ayubu 9:1-35 ONEN
[1] Kisha Ayubu akajibu: [2] “Naam, najua hili ni kweli. Lakini mwanadamu awezaje kuwa mwadilifu mbele za Mungu? [3] Ingawa mtu angetaka kushindana naye, asingaliweza kumjibu Mungu hata mara moja miongoni mwa elfu moja. [4] Hekima yake ni kubwa sana na ana uwezo mwingi mno. Ni nani aliyempinga naye akawa salama? [5] Aiondoa milima bila yenyewe kujua na kuipindua kwa hasira yake. [6] Aitikisa dunia kutoka mahali pake na kuzifanya nguzo zake zitetemeke. [7] Husema na jua, nalo likaacha kuangaza; naye huizima mianga ya nyota. [8] Yeye peke yake huzitandaza mbingu na kuyakanyaga mawimbi ya bahari. [9] Yeye ndiye Muumba wa nyota za Dubu, na Orioni, Kilimia, na makundi ya nyota za kusini. [10] Hutenda maajabu yasiyopimika, miujiza isiyoweza kuhesabiwa. [11] Anapopita karibu nami, siwezi kumwona; apitapo mbele yangu, simtambui. [12] Anapochukua kwa ghafula, ni nani awezaye kumzuia? Ni nani awezaye kumwambia, ‘Unafanya nini?’ [13] Mungu hataizuia hasira yake; hata jeshi kubwa la Rahabu lenye nguvu linajikunyata miguuni pake. [14] “Ni vipi basi mimi nitaweza kubishana naye? Nawezaje kupata maneno ya kuhojiana naye? [15] Ingawa sikuwa na hatia, sikuweza kumjibu; ningeweza tu kumsihi Mhukumu wangu anihurumie. [16] Hata kama ningemwita kwenye shauri, naye akakubali, siamini kama angenisikiliza. [17] Yeye angeniangamiza kwa dhoruba na kuongeza majeraha yangu pasipo na sababu. [18] Asingeniacha nipumue bali angenifunika kabisa na huzuni kuu. [19] Kama ni suala la nguvu, yeye ni mwenye nguvu! Kama ni suala la haki, ni nani awezaye kumwita mahakamani? [20] Hata kama sikuwa na hatia, kinywa changu kingenihukumu; kama sikuwa na kosa, kingenitangaza kuwa mwenye hatia. [21] “Ingawa mimi sina kosa, haileti tofauti katika nafsi yangu; nauchukia uhai wangu. [22] Hayo yote ni sawa; ndiyo sababu nasema, ‘Yeye huwaangamiza wasio na makosa pamoja na waovu.’ [23] Wakati pigo liletapo kifo cha ghafula, yeye hudhihaki kule kukata tamaa kwa yule asiye na kosa. [24] Wakati nchi inapoangukia mikononi mwa waovu, yeye huwafunga macho mahakimu wake. Kama si yeye, basi ni nani? [25] “Siku zangu zapita mbio kuliko mkimbiaji; zinapita upesi bila kuona furaha hata kidogo. [26] Zinapita upesi kama mashua ya mafunjo, mfano wa tai ayashukiaye mawindo kwa ghafula. [27] Kama nikisema, ‘Nitayasahau malalamiko yangu, nitabadili sura ya uso wangu na kutabasamu,’ [28] bado ninahofia mateso yangu yote, kwa kuwa ninajua hutanihesabu kuwa sina hatia. [29] Kwa kuwa nimeonekana mwenye hatia, kwa nini basi nitaabishwe bure? [30] Hata kama ningejiosha kwa sabuni na kutakasa mikono yangu kwa magadi, [31] wewe ungenitupa kwenye shimo la utelezi kiasi kwamba hata nguo zangu zingenichukia sana. [32] “Yeye si mwanadamu kama mimi ili niweze kumjibu, ili kwamba tuweze kushindana naye mahakamani. [33] Laiti angelikuwepo mtu wa kutupatanisha kati yetu, aweke mkono wake juu yetu sote wawili, [34] mtu angeliiondoa fimbo ya Mungu juu yangu, ili utisho wake usiendelee kunitia hofu. [35] Ndipo ningenena naye, bila kumwogopa, lakini kama ilivyo kwangu sasa, sitaweza.
