[1] “Nayachukia sana haya maisha yangu; kwa hiyo nitatoa malalamiko yangu kwa wazi bila kujizuia, nami nitanena kutokana na uchungu wa moyo wangu. [2] Nitamwambia Mungu: Usinihukumu, bali niambie una mashtaka gani dhidi yangu. [3] Je, inakupendeza wewe kunionea, kuikataa kwa dharau kazi ya mikono yako, huku wewe ukitabasamu juu ya mipango ya waovu? [4] Je, wewe una macho ya kimwili? Je, wewe huona kama mwanadamu aonavyo? [5] Je, siku zako ni kama zile za mwanadamu, au miaka yako ni kama ile ya mtu, [6] ili kwamba utafute makosa yangu na kuichunguza dhambi yangu; [7] ingawa wajua kuwa mimi sina hatia, na hakuna awezaye kunitoa mkononi mwako? [8] “Mikono yako ndiyo iliyoniumba na kunifanya. Je, sasa utageuka na kuniangamiza? [9] Kumbuka kuwa ulinifinyanga kama udongo wa mfinyanzi. Je, sasa utanifanya kuwa mavumbi tena? [10] Je, wewe hukunimimina mimi kama maziwa, na kunigandisha kama jibini, [11] ukanivika ngozi na nyama, na kuniunga pamoja kwa mifupa na mishipa? [12] Umenipa uhai na kunitendea wema, katika uangalizi wako umeilinda roho yangu. [13] “Lakini hili ndilo ulilolificha moyoni mwako, nami ninajua kuwa hili lilikuwa katika nia yako: [14] Kama nilifanya dhambi, ungekuwa umeniona, wala usingeacha kosa langu lipite bila kuadhibiwa. [15] Kama nina hatia, ole wangu! Hata kama ningekuwa sina hatia, siwezi kukiinua kichwa changu, kwa kuwa nimejawa na aibu, na kuzama katika mateso yangu. [16] Kama nikiinua kichwa changu juu, unaninyatia kama simba, na kuonyesha tena uwezo wa kutisha dhidi yangu. [17] Wewe waleta mashahidi wapya dhidi yangu na kuzidisha hasira yako juu yangu; nazo nguvu zako zinanijia wimbi moja baada ya jingine. [18] “Kwa nini basi ulinitoa tumboni? Ninatamani ningekufa kabla jicho lolote halijaniona. [19] Laiti nisingekuwako kamwe, au ningekuwa nimechukuliwa moja kwa moja kutoka tumboni kwenda kaburini! [20] Je, siku zangu chache si zimekaribia kuisha? Niachie ili niweze kupata muda mfupi wa kufurahi [21] kabla sijaenda mahali ambapo hakuna kurudi tena, katika nchi ya giza na uvuli wa mauti, [22] nchi ya giza kuu sana, yenye uvuli wa giza na machafuko, mahali ambapo hata nuru ni giza.”