[1] Kisha Bildadi Mshuhi akajibu: [2] “Hata lini wewe utasema mambo kama haya? Maneno yako ni kama upepo mkuu. [3] Je, Mungu hupotosha hukumu? Je, Mwenyezi hupotosha kile kilicho haki? [4] Watoto wako walipomtenda dhambi, aliwapa adhabu ya dhambi yao. [5] Lakini ukimtafuta Mungu, nawe ukamsihi Mwenyezi, [6] ikiwa wewe ni safi na mnyofu, hata sasa atainuka mwenyewe kwa niaba yako, na kukurudisha katika mahali pako pa haki. [7] Ijapokuwa mwanzo wako ulikuwa mdogo, lakini mwisho wako utakuwa wa mafanikio. [8] “Ukaulize vizazi vilivyotangulia na uone baba zao walijifunza nini, [9] kwa kuwa sisi tumezaliwa jana tu na hatujui lolote, nazo siku zetu duniani ni kama kivuli tu. [10] Je, hawatakufundisha na kukueleza? Je, hawataleta maneno kutoka kwenye kufahamu kwao? [11] Je, mafunjo yaweza kumea mahali pasipo na matope? Matete yaweza kustawi bila maji? [12] Wakati bado yanaendelea kukua kabla ya kukatwa, hunyauka haraka kuliko majani mengine. [13] Huu ndio mwisho wa watu wote wanaomsahau Mungu; vivyo hivyo matumaini ya wasiomjali Mungu huangamia. [14] Lile analolitumainia huvunjika upesi; lile analolitegemea ni utando wa buibui. [15] Huutegemea utando wake, lakini hausimami; huungʼangʼania, lakini haudumu. [16] Yeye ni kama mti ulionyeshewa vizuri wakati wa jua, ukieneza machipukizi yake bustanini; [17] huifunganisha mizizi yake kwenye lundo la mawe, na kutafuta nafasi katikati ya mawe. [18] Unapongʼolewa kutoka mahali pake, ndipo mahali pale huukana na kusema, ‘Mimi kamwe sikukuona.’ [19] Hakika uhai wake hunyauka, na kutoka udongoni mimea mingine huota. [20] “Hakika Mungu hamkatai mtu asiye na hatia, wala kuitia nguvu mikono ya mtenda mabaya. [21] Bado atakijaza kinywa chako na kicheko, na midomo yako na kelele za shangwe. [22] Adui zako watavikwa aibu, nazo hema za waovu hazitakuwepo tena.”