Ayubu 7:1-21 ONEN

[1] “Je, mwanadamu hana kazi ngumu duniani? Siku zake si kama zile za mtu aliyeajiriwa? [2] Kama mtumwa anavyovionea shauku vivuli vya jioni, au mtu aliyeajiriwa anavyoungojea mshahara wake, [3] ndivyo nilivyogawiwa miezi ya ubatili, nami nimeandikiwa huzuni usiku hata usiku. [4] Wakati nilalapo ninawaza, ‘Itachukua muda gani kabla sijaamka?’ Usiku huwa mrefu, nami najigeuzageuza hadi mapambazuko. [5] Mwili wangu umevikwa mabuu na uchafu, ngozi yangu imetumbuka na kutunga usaha. [6] “Siku zangu zinapita upesi kuliko mtande wa kufuma, nazo zinafikia mwisho wake bila matumaini. [7] Kumbuka, Ee Mungu, maisha yangu ni kama pumzi; macho yangu kamwe hayataona tena raha. [8] Lile jicho linaloniona sasa halitaniona tena; utanitafuta, wala sitakuwepo. [9] Kama vile wingu liondokavyo na kutoweka, vivyo hivyo yeye ashukaye kaburini harudi tena. [10] Kamwe harudi tena nyumbani mwake; wala mahali pake hapatamjua tena. [11] “Kwa hiyo sitanyamaza; nitanena kutokana na maumivu makuu ya roho yangu, nitalalama kwa uchungu wa nafsi yangu. [12] Je, mimi ni bahari, au mnyama mkubwa mno akaaye vilindini, hata uniweke chini ya ulinzi? [13] Ninapofikiri kwamba kitanda changu kitanifariji, nacho kiti changu cha fahari kitapunguza malalamiko yangu, [14] ndipo wanitisha kwa ndoto na kunitia hofu kwa maono, [15] hivyo ninachagua kujinyonga na kufa, kuliko huu mwili wangu. [16] Ninayachukia maisha yangu; nisingetamani kuendelea kuishi. Niache; siku zangu ni ubatili. [17] “Mwanadamu ni kitu gani hata umjali kiasi hiki, kwamba unamtia sana maanani, [18] kwamba unamwangalia kila asubuhi na kumjaribu kila wakati? [19] Je, hutaacha kamwe kunitazama, au kuniacha japo kwa kitambo kidogo tu? [20] Ikiwa nimetenda dhambi, nimekufanyia nini, Ewe mlinzi wa wanadamu? Kwa nini umeniweka niwe shabaha yako? Je, nimekuwa mzigo kwako? [21] Kwa nini husamehi makosa yangu na kuachilia dhambi zangu? Kwa kuwa hivi karibuni nitalala mavumbini; nawe utanitafuta, wala sitakuwepo.”

About this translation

Life Bible app icon
Get the Life Bible app Read offline, sync highlights and notes, and study with your library on any device.