Ayubu 6:1-30 ONEN
[1] Kisha Ayubu akajibu: [2] “Laiti uchungu wangu ungeweza kupimwa, nayo taabu yangu yote ingewekwa kwenye mizani! [3] Kwa kuwa hakika ingekuwa nzito kuliko mchanga wa bahari zote, kwa hiyo si ajabu maneno yangu yamekuwa ya haraka. [4] Mishale ya Mwenyezi iko ndani yangu, roho yangu inakunywa sumu yake; vitisho vya Mungu vimejipanga dhidi yangu. [5] Je, punda-mwitu hulia akiwa na majani, au ngʼombe dume hulia akiwa na chakula? [6] Je, chakula kisicho na ladha huliwa bila chumvi, au upo utamu katika ute mweupe wa yai? [7] Ninakataa kuvigusa; vyakula vya aina hii hunichukiza. [8] “Laiti ningepata haja yangu, kwamba Mungu angenijalia hilo nililotarajia, [9] kwamba Mungu angekuwa radhi kuniponda, kuuachia mkono wake na kunikatilia mbali! [10] Ndipo bado ningekuwa na hii faraja, furaha yangu katika maumivu makali: kwamba sikuwa nimeyakana maneno yake yeye Aliye Mtakatifu. [11] “Ninazo nguvu gani, hata niendelee kutumaini? Matazamio yangu ya mbele ni nini, hata niendelee kuwa mvumilivu? [12] Je, mimi nina nguvu za jiwe? Je, mwili wangu ni shaba? [13] Je, ninao uwezo wowote wa kujisaidia mimi mwenyewe, wakati ambapo mafanikio yamefukuziwa mbali nami? [14] “Mtu anayekata tamaa angetazamia moyo wa kujitoa wa rafiki zake, hata kama akiacha uchaji wa Mwenyezi. [15] Lakini ndugu zangu sio wa kutegemewa, ni kama vijito vya msimu, ni kama vijito ambavyo hufurika [16] wakati vimefunikwa barafu iyeyukayo, ambavyo hujazwa na theluji inayoyeyuka, [17] lakini hukauka majira ya ukame, na wakati wa hari hutoweka katika mikondo yake. [18] Misafara hugeuka kutoka njia zake; hukwea kwenda kwenye nchi ya ukiwa na kuangamia. [19] Misafara ya Tema inatafuta maji, wafanyabiashara wa Sheba wanaosafiri hutazama kwa matarajio. [20] Wamedhikika, kwa sababu walikuwa na matumaini; wanafika huko, lakini wanahuzunika kwa kukosa walichotarajia. [21] Sasa nanyi mmethibitika kwamba hamna msaada wowote; mnaona jambo la kutisha, nanyi mnaogopa. [22] Je, nimewahi kusema, ‘Toeni kitu kwa ajili yangu, au mnilipie fidia kutoka mali zenu, [23] au niokoeni mikononi mwa adui, au nikomboeni kutoka makucha ya wasio na huruma’? [24] “Nifundisheni, nami nitanyamaza kimya; nionyesheni nilikokosea. [25] Tazama yalivyo ya kuumiza maneno ya kweli! Lakini mabishano yenu yanathibitisha nini? [26] Je, mna maana ya kuyasahihisha ninayosema, na kuyafanya maneno ya mtu anayekata tamaa kama upepo? [27] Mngeweza hata kupiga kura kwa ajili ya yatima, na kubadilishana rafiki yenu na mali. [28] “Lakini sasa kuweni na huruma mkaniangalie mimi. Je, ningeweza kusema uongo mbele zenu? [29] Tulizeni hasira, msiwe wadhalimu; angalieni tena, kwa maana nimehatarisha uadilifu wangu. [30] Je, pana uovu wowote midomoni mwangu? Je, kinywa changu hakiwezi kupambanua hila?
