[1] “Ita kama unataka, lakini ni nani atakayekujibu? Ni yupi kati ya hao watakatifu utakayemgeukia? [2] Kuweka uchungu moyoni humuua mpumbavu, nao wivu humchinja mjinga. [3] Mimi mwenyewe nimemwona mpumbavu akistawi, lakini ghafula nyumba yake ikawa imelaaniwa. [4] Watoto wake wako mbali na usalama, hushindwa mahakamani bila mtetezi. [5] Wenye njaa huyala mavuno yake, wakiyatoa hata katikati ya miiba, nao wenye kiu huitamani sana mali yake. [6] Kwa maana taabu haioti kutoka kwenye udongo, wala udhia hauchipui kutoka ardhini. [7] Lakini mwanadamu huzaliwa ili kutaabika, kwa hakika kama cheche za moto zirukavyo kuelekea juu. [8] “Lakini ingekuwa ni mimi, ningemlalamikia Mungu, ningeliweka shauri langu mbele zake. [9] Yeye hutenda maajabu yasiyoweza kutambuliwa, miujiza isiyoweza kuhesabika. [10] Yeye huipa nchi mvua, huyapeleka maji kunyesha mashamba. [11] Huwainua juu wanyonge, nao wale waombolezao huinuliwa wakawa salama. [12] Huipinga mipango ya wenye hila, ili mikono yao isifikie ufanisi. [13] Yeye huwanasa wenye hekima katika hila yao, nayo mipango ya wadanganyifu huifagilia mbali. [14] Giza huwapata wakati wa mchana; wakati wa adhuhuri hupapasa kama vile usiku. [15] Humwokoa mhitaji kutokana na upanga ulioko kinywani mwao; huwaokoa kutokana na makucha ya wenye nguvu. [16] Kwa hiyo maskini analo tarajio, nao udhalimu hufumba kinywa chake. [17] “Heri mtu yule ambaye Mungu humrudi; kwa hiyo usidharau adhabu yake Mwenyezi. [18] Kwa kuwa hutia jeraha, lakini pia huyafunga; huumiza, lakini mikono yake pia huponya. [19] Kutoka majanga sita atakuokoa; naam, hata katika saba hakuna dhara litakalokupata wewe. [20] Wakati wa njaa atakukomboa wewe na kifo, naye katika vita atakukomboa na pigo la upanga. [21] Utalindwa kutokana na kichapo cha ulimi, wala hutakuwa na sababu ya kuogopa maangamizi yatakapokujia. [22] Utayacheka maangamizo na njaa, wala hutakuwa na sababu ya kuwaogopa wanyama wakali wa mwituni. [23] Kwa kuwa utakuwa na agano na mawe ya mashamba, nao wanyama wa mwitu watakuwa na amani nawe. [24] Utajua ya kwamba hema lako li salama; utahesabu mali zako wala hutakuta chochote kilichopungua. [25] Utajua ya kuwa watoto wako watakuwa wengi, nao wazao wako wengi kama majani ya nchi. [26] Utaingia kaburini ukiwa na umri wa uzee mtimilifu, kama masuke ya ngano yakusanywapo kwa wakati wake. [27] “Tumelichunguza hili, nalo ni kweli. Hivyo lisikie na ulitendee kazi.”