[1] Ndipo Elifazi Mtemani akajibu: [2] “Kama mtu akithubutu kuzungumza nawe, kutakukasirisha? Lakini ni nani awezaye kujizuia asiseme? [3] Fikiri jinsi ambavyo umewafundisha watu wengi, jinsi ambavyo umeitia nguvu mikono iliyokuwa dhaifu. [4] Maneno yako yamewategemeza wale waliojikwaa; umeyatia nguvu magoti yaliyokuwa dhaifu. [5] Lakini sasa hii taabu imekujia wewe, nawe unashuka moyo; imekupiga wewe, nawe unafadhaika. [6] Je, kumcha Mungu kwako hakupaswi kuwa ndiyo matumaini yako na njia zako kutokuwa na lawama ndilo taraja lako? [7] “Fikiri sasa: Ni mtu yupi asiye na hatia ambaye aliwahi kuangamia? Ni wapi wanyofu waliwahi kuangamizwa? [8] Kwa jinsi ambavyo mimi nimechunguza, wale walimao ubaya na wale hupanda uovu, huvuna hayo hayo hayo. [9] Kwa pumzi ya Mungu huangamizwa; kwa mshindo wa hasira zake huangamia. [10] Simba anaweza kunguruma na kukoroma, lakini bado meno ya simba mkubwa huvunjika. [11] Simba anaweza kuangamia kwa kukosa mawindo, nao wana wa simba jike hutawanyika. [12] “Neno lililetwa kwangu kwa siri, masikio yangu yakasikia mnongʼono wake. [13] Katikati ya ndoto za kutia wasiwasi wakati wa usiku, hapo usingizi mzito uwapatapo wanadamu, [14] hofu na kutetemeka kulinishika na kufanya mifupa yangu yote itetemeke. [15] Kuna roho aliyepita mbele ya uso wangu, nazo nywele za mwili wangu zikasimama. [16] Yule roho akasimama, lakini sikuweza kutambua kilikuwa kitu gani. Umbo fulani lilisimama mbele ya macho yangu, kukawa na ukimya kisha nikasikia sauti: [17] ‘Je, binadamu aweza kuwa mwadilifu kuliko Mungu? Je, mtu aweza kuwa safi kuliko Muumba wake? [18] Kama Mungu hawaamini watumishi wake, kama yeye huwalaumu malaika zake kwa kukosea, [19] ni mara ngapi zaidi wale waishio katika nyumba za udongo wa mfinyanzi, ambazo misingi yake ipo mavumbini, ambao wamepondwa kama nondo! [20] Kati ya mawio na machweo huvunjwa vipande vipande; bila yeyote kutambua, huangamia milele. [21] Je, kamba za hema yao hazikungʼolewa, hivyo hufa bila hekima?’