[1] BWANA akamwambia Ayubu: [2] “Je, mwenye kushindana na Mwenyezi aweza kumsahihisha? Mwenye kumlaumu Mungu na ajibu.” [3] Ndipo Ayubu akamjibu BWANA: [4] “Mimi sistahili kabisa: ninawezaje kukujibu wewe? Nauweka mkono wangu juu ya kinywa changu. [5] Nimesema mara moja, lakini sina jibu; naam, nimesema mara mbili, lakini sitasema tena.” [6] Ndipo BWANA akasema na Ayubu kutoka upepo wa kisulisuli: [7] “Jikaze kama mwanaume; nitakuuliza maswali, nawe yakupasa unijibu. [8] “Je, utabatilisha hukumu yangu? Utanilaumu mimi ili kujihesabia haki mwenyewe? [9] Je, una mkono kama wa Mungu, nawe waweza kutoa sauti ya ngurumo kama yake? [10] Basi jivike mwenyewe utukufu na fahari, nawe uvae heshima na enzi. [11] Fungulia ukali wa ghadhabu yako, mtafute kila mwenye kiburi umshushe, [12] mwangalie kila mtu mwenye kiburi na umnyenyekeze, waponde waovu mahali wasimamapo. [13] Wazike wote mavumbini pamoja; wafunge nyuso zao kaburini. [14] Ndipo mimi mwenyewe nitakukubalia kuwa mkono wako mwenyewe wa kuume unaweza kukuokoa. [15] “Mwangalie mnyama aitwaye Behemothi, niliyemuumba kama nilivyokuumba wewe, anayekula majani kama ngʼombe. [16] Tazama basi nguvu alizo nazo kwenye viuno vyake, uwezo alio nao kwenye misuli ya tumbo lake! [17] Mkia wake hutikisika kama mwerezi; mishipa ya mapaja yake imesukwa pamoja. [18] Mifupa yake ni bomba za shaba, maungo yake ni kama fito za chuma. [19] Yeye ni wa kwanza miongoni mwa kazi za Mungu, lakini Muumba wake anaweza kumsogelea kwa upanga wake. [20] Vilima humletea yeye mazao yake, nao wanyama wote wa porini hucheza karibu naye. [21] Hulala chini ya mimea ya yungiyungi, katika maficho ya matete kwenye matope. [22] Hiyo mimea ya yungiyungi humficha kwenye vivuli vyake; miti mirefu karibu na kijito humzunguka. [23] Wakati mto ufurikapo, yeye hapati mshtuko wa hofu; yeye yu salama, hata kama Yordani ingefurika hadi kwenye kinywa chake. [24] Je, mtu yeyote anaweza kumkamata yeye akiwa macho, au kumnasa kwa mtego na kutoboa pua yake?