Ayubu 39:1-30 ONEN
[1] “Je, wajua ni wakati gani mbuzi wa mlimani wanapozaa? Je, watambua ni wakati gani kulungu jike azaapo mtoto wake? [2] Je, waweza kuhesabu miezi hadi wazaapo? Je, unajua majira yao ya kuzaa? [3] Wao hujiinamisha na kuzaa watoto wao; utungu wa kuzaa unakoma. [4] Watoto wao hustawi na kuongezeka nguvu nyikani; huenda zao wala hawarudi tena. [5] “Ni nani aliyemwachia punda-mwitu awe huru? Ni nani aliyezifungua kamba zake? [6] Nimempa nchi isiyokaliwa na watu kuwa masikani yake, nchi ya chumvi kuwa makao yake. [7] Huzicheka ghasia za mji, wala hasikii kelele za mwendesha gari. [8] Huzunguka vilimani kwa ajili ya malisho na kutafuta kila kitu kibichi. [9] “Je, nyati atakubali kukutumikia? Atakaa karibu na hori lako usiku? [10] Je, waweza kumfungia kwenye matuta kwa kamba? Je, atalima mabonde nyuma yako? [11] Je, utamtumainia kwa ajili ya nguvu zake nyingi? Utamwachia yeye kazi zako nzito? [12] Utaweza kumwamini akuletee nafaka yako nyumbani kutoka shambani na kuikusanya kwenye sakafu yako ya kupuria? [13] “Mbuni hupigapiga mabawa yake kwa furaha, lakini hayawezi kulinganishwa na mabawa na manyoya ya korongo. [14] Huyataga mayai yake juu ya ardhi, na kuyaacha yapate joto mchangani, [15] bila kujali kuwa mguu waweza kuyaponda, kwamba baadhi ya wanyama wa porini wanaweza kuyakanyaga. [16] Yeye huyafanyia makinda yake ukatili kama vile si yake; hajali kwamba taabu yake inaweza ikawa bure, [17] kwa kuwa Mungu hakumjalia hekima, wala hakumpa fungu la akili njema. [18] Lakini akunjuapo mabawa yake kukimbia, humcheka farasi pamoja na yeye aliyempanda. [19] “Je, wewe humpa farasi nguvu au kuivika shingo yake manyoya marefu? [20] Je, wewe humfanya farasi aruke kama nzige, akistaajabisha kwa tishio la mlio wake wa majivuno? [21] Huparapara bila woga, akizifurahia nguvu zake, husonga mbele kukabiliana na silaha. [22] Huicheka hofu, haogopi chochote, wala haukimbii upanga. [23] Podo hutoa sauti kando yake, pamoja na mkuki unaongʼaa na fumo. [24] Bila woga na kwa ghadhabu huimeza nchi, wala tarumbeta iliapo yeye hawezi kusimama. [25] Asikiapo sauti ya baragumu yeye hulia, ‘Aha!’ Hunusa harufu ya vita toka mbali, sauti ya mtoa amri na ukelele wa vita. [26] “Je, mwewe huruka kwa hekima yako na kuyakunjua mabawa yake kuelekea kusini? [27] Je, tai hupaa juu kwa amri yako na kujenga kiota chake mahali pa juu? [28] Huishi juu ya miamba mirefu na kukaa huko usiku; majabali yenye ncha kali ndiyo ngome yake. [29] Kutoka huko hutafuta chakula chake; macho yake hukiona kutoka mbali. [30] Makinda yake hujilisha damu, na pale palipo na machinjo, ndipo yeye alipo.”
