Ayubu 41:1-34 ONEN
[1] “Je, waweza kumvua Lewiathani kwa ndoano ya samaki, au kufunga ulimi wake kwa kamba? [2] Waweza kupitisha kamba puani mwake, au kutoboa taya lake kwa kulabu? [3] Je, ataendelea kukuomba umhurumie? Atasema nawe maneno ya upole? [4] Je, atafanya agano nawe ili umtwae awe mtumishi wako maisha yake yote? [5] Je, utamfuga na kumfanya rafiki kama ndege, au kumfunga kamba kwa ajili ya wasichana wako? [6] Je, wafanyabiashara watabadilishana bidhaa kwa ajili yake? Watamgawanya miongoni mwa wafanyao biashara? [7] Je, waweza kuijaza ngozi yake kwa vyuma vyenye ncha kali, au kichwa chake kwa mkuki wa kuvulia samaki? [8] Kama ukiweka mkono wako juu yake, utavikumbuka hivyo vita na kamwe hutarudia tena! [9] Tumaini lolote la kumtiisha ni kujidanganya; kule kumwona tu kunamwangusha mtu chini. [10] Hakuna yeyote aliye mkali athubutuye kumchokoza. Ni nani basi awezaye kusimama dhidi yangu? [11] Ni nani mwenye madai dhidi yangu ili nipate kumlipa? Kila kitu kilicho chini ya mbingu ni mali yangu. [12] “Sitashindwa kunena juu ya maungo yake, nguvu zake na umbo lake zuri. [13] Ni nani awezaye kumvua gamba lake la nje? Ni nani awezaye kumsogelea na lijamu? [14] Nani athubutuye kuufungua mlango wa kinywa chake, kilichozungukwa na meno yake ya kutisha pande zote? [15] Mgongo wake una safu za ngao zilizoshikamanishwa imara pamoja; [16] kila moja iko karibu sana na mwenzake, wala hakuna hewa iwezayo kupita kati yake. [17] Zimeunganishwa imara kila moja na nyingine; zimengʼangʼaniana pamoja wala haziwezi kutenganishwa. [18] Akipiga chafya mwanga humetameta; macho yake ni kama mionzi ya mapambazuko. [19] Mienge iwakayo humiminika kutoka kinywani mwake; cheche za moto huruka nje. [20] Moshi hufuka kutoka puani mwake, kama kutoka kwenye chungu kinachotokota kwa moto wa matete. [21] Pumzi yake huwasha makaa ya mawe, nayo miali ya moto huruka kutoka kinywani mwake. [22] Nguvu hukaa katika shingo yake; utisho hutangulia mbele yake. [23] Mikunjo ya nyama yake imeshikamana imara pamoja; iko imara na haiwezi kuondolewa. [24] Kifua chake ni kigumu kama mwamba, kigumu kama jiwe la chini la kusagia. [25] Ainukapo, mashujaa wanaogopa; hurudi nyuma mbele yake anapokwenda kwa kishindo. [26] Upanga unaomfikia haumdhuru, wala mkuki au mshale wala fumo. [27] Chuma hukiona kama unyasi, na shaba kama mti uliooza. [28] Mishale haimfanyi yeye akimbie; mawe ya kombeo kwake ni kama makapi. [29] Rungu kwake huwa kama kipande cha jani kavu; hucheka sauti za kugongana kwa mkuki. [30] Sehemu zake za chini kwenye tumbo zina menomeno na mapengo kama vigae vya chungu, zikiacha mburuzo kwenye matope kama chombo chenye meno cha kupuria. [31] Huvisukasuka vilindi kama sufuria kubwa ichemkayo, na kukoroga bahari kama chungu cha marhamu. [32] Anapopita nyuma yake huacha mkondo unaometameta; mtu angedhani vilindi vilikuwa na mvi. [33] Hakuna chochote duniani kinacholingana naye: yeye ni kiumbe kisicho na woga. [34] Yeye huwatazama chini wale wote wenye kujivuna; yeye ni mfalme juu ya wote wenye kiburi.”
