[1] Baada ya jambo hili, Ayubu akafumbua kinywa chake na kuilaani siku ya kuzaliwa kwake. [2] Kisha akasema: [3] “Siku ya kuzaliwa kwangu na ipotelee mbali, nao usiku ule iliposemekana, ‘Mtoto wa kiume amezaliwa!’ [4] Siku ile na iwe giza; Mungu juu na asiiangalie; nayo nuru isiiangazie. [5] Giza na kivuli kikuu kiikalie tena; wingu na likae juu yake; weusi na uifunike nuru yake. [6] Usiku ule na ushikwe na giza kuu; usihesabiwe katika siku za mwaka, wala usihesabiwe katika siku za mwezi wowote. [7] Usiku ule na uwe tasa; sauti ya furaha na isisikike ndani yake. [8] Wale wazilaanio siku wailaani hiyo siku, wale walio tayari kumwamsha Lewiathani. [9] Nyota zake za alfajiri na ziwe giza; nao ungojee mwanga bila mafanikio, wala usiuone mwonzi wa kwanza wa mapambazuko, [10] kwa sababu huo usiku haukunifungia mlango wa tumbo la mama yangu, ili kuyaficha macho yangu kutokana na taabu. [11] “Kwa nini sikuangamia wakati wa kuzaliwa? Kwa nini sikufa nilipokuwa ninatoka tumboni? [12] Kwa nini pakawa na magoti ya kunipokea na matiti ili nipate kunyonyeshwa? [13] Kwa maana sasa ningekuwa nimepumzika kwa amani. Ningekuwa nimelala na kupumzika [14] pamoja na wafalme na washauri wa dunia, waliojijengea mahali ambapo sasa ni magofu, [15] pamoja na watawala waliokuwa na dhahabu, waliozijaza nyumba zao kwa fedha. [16] Au kwa nini sikufichwa ardhini kama mtoto aliyezaliwa mfu, kama mtoto mchanga ambaye kamwe hakuuona mwanga? [17] Huko waovu huacha kusumbua na huko waliochoka hupumzika. [18] Wafungwa nao hufurahia utulivu wao, hawasikii tena sauti ya kukemea ya kiongozi wa watumwa. [19] Wadogo na wakubwa wamo humo, na mtumwa ameachiwa huru kutoka kwa bwana wake. [20] “Mbona nuru inawaangazia wale walio taabuni, na hao wenye uchungu kupewa uhai, [21] wale wanaotamani kifo ambacho hakiji, wale watafutao kufa zaidi ya kutafuta hazina iliyofichwa, [22] ambao hujawa na furaha, na hushangilia wafikapo kaburini? [23] Kwa nini uhai hupewa mtu ambaye njia yake imefichika, ambaye Mungu amemzungushia boma? [24] Kwa maana kulia kwangu kwa uchungu kwanijia badala ya chakula; kusononeka kwangu kunamwagika kama maji. [25] Lile nililokuwa naliogopa limenijia; lile nililokuwa ninalihofia limenipata. [26] Sina amani, wala utulivu; sina pumziko, bali taabu tu.”