Ayubu 38:1-41 ONEN
[1] Kisha BWANA akamjibu Ayubu kutoka upepo wa kisulisuli. Akasema: [2] “Nani huyu atiaye mashauri yangu giza kwa maneno yasiyo na maarifa? [3] Jikaze kama mwanaume; nitakuuliza swali, nawe unijibu. [4] “Ulikuwa wapi nilipoweka misingi ya dunia? Niambie, kama unafahamu. [5] Ni nani aliyeweka alama vipimo vyake? Hakika wewe unajua! Ni nani aliyenyoosha kamba ya kupimia juu yake? [6] Je, misingi yake iliwekwa juu ya nini, au ni nani aliyeweka jiwe la pembeni, [7] wakati nyota za asubuhi zilipoimba pamoja, na malaika wote walipokuwa wakipiga kelele kwa furaha? [8] “Ni nani aliyeifungia bahari milango ilipopasuka kutoka tumbo, [9] nilipoyafanya mawingu kuwa vazi lake, na kuyafungia katika giza nene, [10] nilipoamuru mipaka yake, na kuiweka milango yake na makomeo mahali pake, [11] niliposema, ‘Unaweza kufika mpaka hapa wala si zaidi; hapa ndipo mawimbi yako yenye kiburi yatakapokomea’? [12] “Umepata kuiamrisha asubuhi ipambazuke, au kuyaonyesha mapambazuko mahali pake, [13] yapate kushika miisho ya dunia, na kuwakungʼuta waovu waliomo? [14] Dunia hubadilika kama udongo wa mfinyanzi chini ya lakiri; sura yake hukaa kama ile ya vazi. [15] Waovu huzuiliwa nuru yao, nao mkono wao ulioinuliwa huvunjwa. [16] “Je, umepata kufika kwenye chemchemi za bahari? Au kutembea mahali pa ndani pa vilindi? [17] Umewahi kuonyeshwa malango ya mauti? Umewahi kuiona milango ya uvuli wa mauti? [18] Je, wewe unafahamu ukubwa wa dunia? Niambie kama unajua haya yote. [19] “Njia ya kufika kwenye makao ya nuru ni ipi? Nako maskani mwa giza ni wapi? [20] Je, unaweza kuvirudisha kwenye makao yake? Unajua njia za kufika maskani mwake? [21] Hakika unajua, kwa kuwa ulikuwa umeshazaliwa! Kwani umeishi miaka mingi! [22] “Je, umeshawahi kuingia katika ghala za theluji, au kuona ghala za mvua ya mawe, [23] ambazo nimeziweka akiba kwa ajili ya wakati wa taabu, na kwa ajili ya wakati wa vita na mapigano? [24] Ni ipi njia iendayo mahali umeme wa radi unapotawanyiwa, au mahali upepo wa mashariki unaposambaziwa juu ya dunia? [25] Ni nani aliyepasua mifereji kwa ajili ya maji mengi ya mvua yaendayo kasi na njia ya umeme wa radi, [26] ili kusababisha mvua kunyeshea mahali pasipokaliwa na mtu, jangwa lisilo na yeyote ndani yake, [27] ili kuitosheleza nchi ya ukiwa na jangwa, na majani yaanze kumea ndani yake? [28] Je, mvua ina baba? Ni nani baba azaaye matone ya umande? [29] Barafu inatoka tumbo la nani? Ni nani azaaye ukungu kutoka mbinguni, [30] wakati maji yawapo magumu kama jiwe, wakati uso wa vilindi vya maji unapoganda? [31] “Je, waweza kuufunga mnyororo wa Kilimia? Waweza kulegeza kamba za Orioni? [32] Waweza kuyaongoza makundi ya nyota kwa majira yake, au kuongoza Dubu na watoto wake? [33] Je, unajua sheria zinazotawala mbingu? Waweza kuweka utawala wa Mungu duniani? [34] “Waweza kuiinua sauti yako mpaka mawinguni, na kujifunika mwenyewe na gharika ya maji? [35] Je, wewe hutuma umeme wa radi kwenye njia zake? Je, hutoa taarifa kwako kukuambia, ‘Sisi tuko hapa’? [36] Ni nani aliyeujalia moyo hekima au kuzipa akili ufahamu? [37] Nani mwenye hekima ya kuyahesabu mawingu? Ni nani awezaye kuinamisha magudulia ya mbinguni [38] wakati mavumbi yawapo magumu, na mabonge ya udongo kushikamana pamoja? [39] “Je, utamwindia simba jike mawindo, na kuwashibisha simba wenye njaa [40] wakati wao wamejikunyata mapangoni mwao, au wakivizia kichakani? [41] Ni nani ampaye kunguru chakula wakati makinda yake yanamlilia Mungu, yakizungukazunguka kwa ajili ya kukosa chakula?
