[1] “Kwa hili moyo wangu unatetemeka, nao unaruka kutoka mahali pake. [2] Sikiliza! Sikiliza ngurumo ya sauti yake, sauti ya ngurumo itokayo kinywani mwake. [3] Huuachilia umeme wake wa radi chini ya mbingu yote na kuupeleka hata miisho ya dunia. [4] Baada ya hayo huja sauti ya ngurumo yake; Mungu hunguruma kwa sauti yake ya fahari. Wakati sauti yake ingurumapo tena, huuachilia umeme wake wa radi. [5] Sauti ya Mungu hunguruma kwa namna za ajabu; yeye hutenda mambo makuu kupita ufahamu wetu. [6] Huiambia theluji, ‘Anguka juu ya dunia,’ nayo manyunyu ya mvua, ‘Uwe mvua ya nguvu.’ [7] Ili wanadamu wote aliowaumba wapate kujua kazi zake, yeye humzuilia kila mtu shughuli zake. [8] Wanyama hujificha; hubakia kwenye mapango yao. [9] Dhoruba hutoka katika chumba chake, baridi hutoka katika upepo uendao kasi. [10] Pumzi ya Mungu hutoa barafu, eneo kubwa la maji huganda. [11] Huyasheheneza mawingu kwa maji, naye husambaza umeme wake wa radi kupitia hayo. [12] Nayo mawingu huzungukazunguka pande zote kwa amri yake, juu ya uso wa dunia yote, kufanya lolote ayaamuruyo. [13] Huleta mawingu ili kuadhibu wanadamu, au kuinyeshea dunia yake na kuonyesha upendo wake. [14] “Ayubu, sikiliza hili; nyamaza na uyafikiri maajabu ya Mungu. [15] Je, unajua jinsi Mungu anavyoyaongoza mawingu, na kufanya umeme wake wa radi utoe mwanga? [16] Je, wajua jinsi mawingu yanavyokaa yakiwa yametulia, hayo maajabu yake yeye aliye mkamilifu katika maarifa? [17] Wewe unayeshindwa na joto katika nguo zako wakati nchi imenyamazishwa kimya bila upepo wa kusini, [18] je, waweza kuungana naye katika kuzitandaza anga, zilizo ngumu kama kioo cha shaba ya kuyeyushwa? [19] “Tuambieni yatupasayo kumwambia; hatuwezi kutayarisha shauri letu kwa sababu ya ujinga wetu. [20] Je, aambiwe kwamba nataka kuongea? Je, yuko mtu ambaye angeomba kumezwa? [21] Basi hakuna awezaye kulitazama jua, jinsi linavyongʼaa angani, upepo ukishafagia mawingu. [22] Kutoka kaskazini yeye huja na fahari kuu; Mungu huja katika utukufu wa kutisha. [23] Yeye Mwenyezi hatuwezi kumfikia, naye ametukuzwa katika uweza; katika hukumu zake na haki yake kuu, hataonea. [24] Kwa hiyo, wanadamu mheshimuni, kwa kuwa yeye hamstahi yeyote anayejidhania kuwa ana hekima.”