Ayubu 36:1-33 ONEN
[1] Elihu akaendelea kusema: [2] “Nivumilie kidogo zaidi nami nitakuonyesha kwamba yako mengi zaidi ya kusemwa kwa ajili ya Mungu. [3] Ninayapata maarifa yangu kutoka mbali, nami nitamhesabia haki Muumba wangu. [4] Uwe na hakika kwamba maneno yangu si ya uongo; mmoja aliye mkamilifu katika maarifa yuko pamoja na wewe. [5] “Mungu ni mwenye nguvu, lakini hamdharau mwanadamu; ni mwenye nguvu, naye ni thabiti katika shauri lake. [6] Hawaachi waovu waendelee kuishi, bali huwapa walioteswa haki yao. [7] Yeye haondoi macho yake kwa wenye haki; huwaketisha penye viti vya enzi pamoja na wafalme na kuwatukuza milele. [8] Lakini ikiwa watu wamefungwa kwenye minyororo, wakiwa wameshikiliwa na kamba za mateso, [9] huwaonyesha yale waliyoyatenda, kwamba wametenda dhambi kwa majivuno. [10] Huwafanya wao kusikia maonyo, na huwaagiza kutubu uovu wao. [11] Kama wakitii na kumtumikia, wataishi siku zao zilizobaki katika mafanikio, na miaka yao katika utoshelevu. [12] Lakini wasiposikiliza, wataangamia kwa upanga, nao watakufa pasipo maarifa. [13] “Wasiomcha Mungu moyoni mwao huficha chuki; hata anapowafunga, hawamwombi msaada. [14] Wanakufa wangali vijana, miongoni mwa wanaume hanithi wa mahali pa kuabudia miungu. [15] Bali wao wanaoteseka huwaokoa katika mateso yao, na kuzungumza nao katika dhiki zao. [16] “Yeye anakubembeleza utoke katika mataya ya dhiki, ili kukuweka mahali palipo na nafasi mbali na kizuizi, hadi kwenye meza yako ya faraja iliyojaa vyakula vizuri. [17] Lakini sasa umelemewa na hukumu kwa ajili ya uovu; hukumu na haki vimekukamata. [18] Uwe mwangalifu ili yeyote asikushawishi kwa utajiri; usipotoshwe kwa fungu kubwa la rushwa. [19] Je, utajiri wako hata nguvu zako nyingi vinaweza kukusaidia usiingie kwenye dhiki? [20] Usiutamani usiku uje, ili uwaburute watu mbali na nyumba zao. [21] Jihadhari usigeukie uovu, ambao unaupenda zaidi kuliko mateso. [22] “Mungu ametukuzwa katika nguvu zake. Ni nani aliye mwalimu kama yeye? [23] Ni nani aliyemwelekeza katika njia zake, au kumwambia, ‘Wewe umetenda yasiyo sawa’? [24] Kumbuka kuzitukuza kazi zake, ambazo watu wamezisifu katika wimbo. [25] Wanadamu wote wameiona; watu wanaikazia macho kwa mbali. [26] Tazama jinsi Mungu alivyo mkuu, kupita ufahamu wetu! Hesabu ya miaka yake haitafutiki. [27] “Yeye huvuta juu matone ya maji, ayachujayo kama mvua kutoka kwenye vijito; [28] mawingu huangusha chini maji yake, nayo mvua nyingi huwanyeshea wanadamu. [29] Ni nani ajuaye jinsi ayatandazavyo mawingu, jinsi angurumavyo kutoka hemani mwake. [30] Tazama jinsi anavyotandaza umeme wa radi kumzunguka, naye huvifunika vilindi vya bahari. [31] Hivi ndivyo atawalavyo mataifa, na kuwapa chakula kwa wingi. [32] Huujaza mkono wake kwa umeme wa radi, na kuuagiza kulenga shabaha yake. [33] Ngurumo zake hutangaza dhoruba inayokuja; hata mifugo hujulisha kukaribia kwake.
