[1] Ndipo Elihu akasema: [2] “Je, unadhani hili ni haki? Wewe unasema, ‘Nina haki mbele za Mungu.’ [3] Bado unamuuliza, ‘Ni faida gani nimepata, na imenifaidi nini kwa kutokutenda dhambi?’ [4] “Ningependa nikujibu wewe pamoja na marafiki zako walio pamoja nawe. [5] Tazama juu mbinguni ukaone; yaangalie mawingu yaliyo juu sana juu yako. [6] Je, ukitenda dhambi, inamdhuruje Mungu? Kama dhambi zako zikiwa nyingi, hilo linamfanyia nini Mungu? [7] Kama wewe ni mwadilifu, unampa nini, au yeye anapokea nini mkononi kwako? [8] Uovu wako unamdhuru tu mtu mwingine kama wewe, nayo haki yako inawafaa wanadamu tu. [9] “Wanadamu hulia kwa kulemewa na mateso; huomba msaada kutoka mkono wenye nguvu. [10] Lakini hakuna asemaye, ‘Yuko wapi Mungu Muumba wangu, yeye anifanyaye niimbe usiku, [11] yeye atufundishaye sisi zaidi kuliko wanyama wa dunia, na kutufanya wenye hekima kuliko ndege wa angani?’ [12] Yeye hajibu wakati watu waliapo kwa sababu ya kiburi cha watu waovu. [13] Naam, Mungu hasikilizi maombi yao ya ubatili; Mwenyezi hayazingatii. [14] Si zaidi sana kwamba hatakusikiliza wewe usemapo humwoni, tena ya kwamba shauri lako liko mbele zake na wewe lazima umngojee, [15] pia zaidi, kwamba hasira yake kamwe haiadhibu wala haangalii uovu hata kidogo? [16] Hivyo Ayubu hufumbua kinywa chake kwa maneno yasiyo na maana; anaongea maneno mengi bila maarifa.”