Ayubu 34:1-37 ONEN
[1] Kisha Elihu akasema: [2] “Sikieni maneno yangu, enyi watu wenye hekima; nisikilizeni mimi, ninyi watu wenye maarifa. [3] Kwa kuwa sikio huyajaribu maneno kama vile ulimi uonjavyo chakula. [4] Tujichagulie wenyewe yaliyo sawa, nasi tujifunze pamoja yaliyo mema. [5] “Ayubu anasema, ‘Mimi sina hatia, lakini Mungu ameninyima haki yangu. [6] Ingawa niko sawa, ninaonekana mwongo; nami ingawa sina kosa, kidonda changu hakiponi.’ [7] Ni mtu gani aliye kama Ayubu, anywaye dharau kama maji? [8] Ashirikianaye na watenda mabaya na kuchangamana na watu waovu. [9] Kwa kuwa anasema, ‘Haimfaidi mwanadamu kitu chochote anapojitahidi kumpendeza Mungu.’ [10] “Hivyo nisikilizeni mimi, ninyi watu wenye ufahamu. Kamwe Mungu hatendi uovu, Mwenyezi hafanyi kosa. [11] Humlipa mwanadamu kwa ajili ya lile alilotenda; huleta juu yake kile ambacho matendo yake yanastahili. [12] Ni jambo lisiloweza kufikiriwa kwamba Mungu angefanya makosa, kwamba Mwenyezi angepotosha hukumu. [13] Je, ni nani aliyemtawaza juu ya dunia? Ni nani aliyemweka kuwa mwangalizi wa ulimwengu wote? [14] Kama lilikuwa kusudi la Mungu, naye akaiondoa Roho yake na pumzi yake, [15] wanadamu wote wangeliangamia kwa pamoja, na mtu angerudi mavumbini. [16] “Kama ninyi mnaufahamu, sikieni hili; sikilizeni hili nisemalo. [17] Je, yeye aichukiaye haki aweza kutawala? Je, utamhukumu mwenye haki, Aliye na Nguvu Zote? [18] Je, si ni yeye awaambiaye wafalme, ‘Ninyi hamfai kitu,’ nao watu mashuhuri, ‘Ninyi ni waovu,’ [19] yeye asiyependelea wakuu, wala haonyeshi upendeleo kwa matajiri kuliko maskini, kwa kuwa wote ni kazi ya mikono yake? [20] Wanakufa ghafula, usiku wa manane; watu wanatikiswa nao hupita; wenye nguvu huondolewa bila mkono wa mwanadamu. [21] “Macho yake yanazitazama njia za wanadamu; anaona kila hatua yao. [22] Hakuna mahali penye giza nene, wala uvuli mkubwa, ambapo watenda mabaya wanaweza kujificha. [23] Mungu hana haja ya kumchunguza mtu sana, ili apate kuja mbele zake kwa hukumu. [24] Bila kuuliza huwapondaponda wenye nguvu nyingi na kuwaweka wengine mahali pao. [25] Kwa sababu huyaangalia matendo yao yote, huwaondoa usiku, nao wakaangamia. [26] Anawaadhibu kwa ajili ya uovu wao mahali ambapo kila mmoja ataweza kuwaona, [27] kwa sababu wameacha kumfuata Mungu, nao hawakuiheshimu njia yake hata moja. [28] Wamesababisha kilio cha maskini kifike mbele zake, hivyo akasikia kilio cha wahitaji. [29] Lakini kama akinyamaza kimya, ni nani awezaye kumhukumu? Kama akiuficha uso wake, ni nani awezaye kumwona? Ikiwa ni taifa au mtu mmoja, kwake ni sawa, [30] ili kumzuia mtu mwovu kutawala, au wale ambao huwategea watu mitego. [31] “Kama mwanadamu akimwambia Mungu, ‘Nimekosa lakini sitatenda dhambi tena. [32] Nifundishe nisichoweza kuona; kama nimekukosea, sitafanya hivyo tena.’ [33] Je basi, Mungu atakulipa kwa masharti yako, wakati wewe umekataa kutubu? Yakupasa wewe uamue, wala si mimi; sasa niambie lile ulijualo. [34] “Wanadamu wenye ufahamu husema, wenye hekima wanaonisikia huniambia, [35] ‘Ayubu huongea bila maarifa; maneno yake hayana busara.’ [36] Laiti Ayubu angejaribiwa hadi kikomo cha mwisho, kwa sababu anajibu kama mtu mwovu! [37] Kwenye dhambi yake huongeza uasi; kwa dharau hupiga makofi miongoni mwetu, na kuzidisha maneno yake dhidi ya Mungu.”
