Ayubu 33:1-33 ONEN
[1] “Lakini Ayubu, sasa, sikiliza maneno yangu; zingatia kila kitu nitakachosema. [2] Karibu nitafungua kinywa changu; maneno yangu yapo katika ncha ya ulimi wangu. [3] Maneno yangu yanatoka katika moyo mnyofu; midomo yangu hunena kwa uaminifu yale niyajuayo. [4] Roho wa Mungu ameniumba; pumzi ya Mwenyezi hunipa uhai. [5] Unijibu basi, kama unaweza; jiandae kunikabili mimi. [6] Mimi ni kama wewe mbele za Mungu; mimi pia nimetolewa kwenye udongo. [7] Huna sababu ya kuniogopa, wala mkono wangu haupaswi kukulemea. [8] “Lakini umesema nikiwa ninakusikia, nami nilisikia maneno yenyewe: [9] ‘Mimi ni safi na sina dhambi; mimi ni safi na sina hatia. [10] Lakini bado Mungu amepata dosari kwangu, naye ananiona kama adui yake. [11] Ananifunga miguu kwa pingu, tena anaziangalia njia zangu zote kwa karibu.’ [12] “Lakini mimi ninakuambia, katika jambo hili wewe una makosa, kwa maana Mungu ni mkuu kuliko mwanadamu. [13] Kwa nini unamlalamikia kwamba yeye hamjibu mwanadamu? [14] Kwa kuwa Mungu husema, wakati huu kwa njia moja, au wakati mwingine kwa njia nyingine, ingawa mwanadamu anaweza asielewe. [15] Mungu husema na mwanadamu katika ndoto, katika maono ya usiku, wakati usingizi mzito uwaangukiapo wanadamu wasinziapo vitandani mwao, [16] anaweza akasemea masikioni mwao, na kuwatia hofu kwa maonyo, [17] ili kumgeuza mtu kutoka kwenye kutenda mabaya na kumwepusha na kiburi, [18] kuiokoa nafsi yake na shimo, uhai wake usiangamizwe kwa upanga. [19] Mtu anaweza kutiwa adabu kwa maumivu kitandani mwake, kwa dhiki za mfululizo katika mifupa yake, [20] kiasi kwamba maisha yake yenyewe yanakataa chakula nayo nafsi yake ikakichukia kabisa hata chakula kizuri. [21] Nyama ya mwili wake huisha kwa kukonda, nayo mifupa yake ambayo mwanzoni ilikuwa imefichika, sasa inatokeza nje. [22] Nafsi yake inakaribia kaburi, nao uhai wake karibu na wajumbe wa kifo. [23] “Kama bado kuna malaika upande wake kama mtetezi, mmoja miongoni mwa elfu, wa kumwambia mwanadamu lililo jema kwake, [24] kumwonea huruma na kusema, ‘Mwokoe asije akatumbukia shimoni; nimepata ukombozi kwa ajili yake’: [25] ndipo nyama ya mwili wake hufanywa mpya kama ya mtoto; hurudishwa upya kama siku za ujana wake. [26] Humwomba Mungu, akapata kibali kwake, huuona uso wa Mungu na kushangilia kwa furaha; Mungu humrudisha katika hali yake ya uadilifu. [27] Ndipo huja mbele za watu na kusema, ‘Nilitenda dhambi na kupotosha kilichokuwa haki, lakini sikuadhibiwa kama nilivyostahili. [28] Alinikomboa nafsi yangu nisitumbukie shimoni, nami nitaishi ili kuufurahia mwanga.’ [29] “Mungu hufanya haya yote kwa mwanadamu; mara mbili hata mara tatu, [30] ili aigeuze nafsi yake toka shimoni, ili nuru ya uzima imwangazie. [31] “Ayubu, zingatia, nisikilize mimi; nyamaza, nami nitanena. [32] Kama unalo lolote la kusema, unijibu; sema, kwa maana ninataka uonekane huna hatia. [33] Lakini kama huna la kusema, basi nisikilize mimi; nyamaza, nami nitakufundisha hekima.”
