[1] Basi watu hawa watatu wakaacha kumjibu Ayubu, kwa kuwa alikuwa mwadilifu machoni pake mwenyewe. [2] Lakini Elihu mwana wa Barakeli, wa kabila la Buzi wa jamaa ya Ramu, akamkasirikia sana Ayubu, kwa sababu ya kujihesabia haki mwenyewe badala ya Mungu. [3] Pia aliwakasirikia hao rafiki watatu wa Ayubu, kwa sababu hawakuweza kupata njia ya kuthibitisha ya kuwa hayo maneno ya Ayubu hayakuwa ya kweli, nao bado walikuwa wamemlaumu. [4] Basi Elihu alikuwa amesubiri kwanza waongee na Ayubu kwa sababu walikuwa na umri mkubwa kumliko yeye. [5] Lakini alipoona watu hao watatu hawakuwa na kitu zaidi cha kusema, hasira yake ikaamka. [6] Basi Elihu mwana wa Barakeli wa kabila la Buzi akasema: “Mimi ni mdogo kwa umri, nanyi ni wazee; ndiyo sababu niliogopa, sikuthubutu kuwaambia kile ninachojua. [7] Nilifikiri, ‘Yafaa umri useme, nao wingi wa miaka ungefundisha hekima.’ [8] Lakini ni Roho iliyoko ndani ya mwanadamu, pumzi ya Mwenyezi, ndiyo impayo yeye ufahamu. [9] Sio wazee peke yao walio na hekima, sio wenye umri mkubwa peke yao wanaofahamu lililo sawa. [10] “Kwa hiyo nasema: Nisikilizeni mimi; mimi nami nitawaambia lile ninalojua. [11] Nilingojea mlipokuwa mnaongea, nilizisikiliza hoja zenu; mlipokuwa mkitafuta maneno ya kusema, [12] niliwasikiliza kwa makini. Lakini hakuna hata mmoja wenu aliyethibitisha kwamba Ayubu amekosa; hakuna hata mmoja wenu aliyeweza kujibu hoja zake. [13] Msiseme, ‘Tumepata hekima; Mungu na amthibitishe kuwa mwongo, wala si mwanadamu.’ [14] Lakini Ayubu hajayapanga maneno yake dhidi yangu, nami sitamjibu kwa kutumia hoja zenu. [15] “Wametiwa hofu na hawana la zaidi la kusema; maneno yamewaishia. [16] Je, ningoje sasa kwa sababu wamekuwa kimya, kwa vile sasa wanasimama bila kuwa na la kujibu? [17] Mimi nami nitakuwa na la kusema; mimi nami nitasema lile nilijualo. [18] Kwa kuwa nimejawa na maneno, nayo Roho iliyomo ndani yangu yanisukuma; [19] ndani yangu niko kama chupa iliyojazwa divai, kama kiriba kipya cha divai kilicho tayari kupasuka. [20] Ni lazima niseme ili niweze kutulia; ni lazima nifumbue midomo yangu nipate kujibu. [21] Sitampendelea mtu yeyote, wala sitajipendekeza kwa mtu yeyote; [22] kwa kuwa kama ningekuwa stadi wa kujipendekeza, Muumba wangu angeniondolea mbali kwa upesi.