Ayubu 31:1-40 ONEN
[1] “Nimefanya agano na macho yangu yasimtazame msichana kwa kumtamani. [2] Kwa kuwa fungu la mwanadamu ni gani kutoka kwa Mungu juu, urithi wake kutoka kwa Mungu Mwenye Nguvu Aliye juu? [3] Je, si uharibifu kwa watu waovu, maangamizi kwa wale watendao mabaya? [4] Je, yeye hazioni njia zangu na kuihesabu kila hatua yangu? [5] “Kama nimeishi katika uongo au mguu wangu umekimbilia udanganyifu, [6] Mungu na anipime katika mizani za uaminifu, naye atajua kwamba sina hatia: [7] kama hatua zangu zimepotoka kutoka kwenye njia, kama moyo wangu umeongozwa na macho yangu, au kama mikono yangu imetiwa unajisi, [8] basi wengine na wale nilichokipanda, nayo yale yote niliyootesha na yangʼolewe. [9] “Kama moyo wangu umeshawishiwa na mwanamke, au kama nimevizia mlangoni mwa jirani yangu, [10] basi mke wangu na asage nafaka ya mwanaume mwingine, nao wanaume wengine walale naye. [11] Kwa kuwa hilo lingekuwa aibu, naam, dhambi ya kuhukumiwa. [12] Ni moto uwakao kwa Uharibifu; ungekuwa umengʼoa mavuno yangu. [13] “Kama ningewanyima haki watumishi wangu wanaume au vijakazi wangu, walipokuwa na manungʼuniko dhidi yangu, [14] nitafanya nini Mungu atakaponikabili? Nitamjibu nini nitakapoitwa kutoa hesabu? [15] Je, yeye aliyeniumba tumboni mwa mama yangu, si ndiye aliwaumba? Je, si ni yeye huyo mmoja aliyetuumba sote ndani ya mama zetu? [16] “Ikiwa nimewanyima maskini haja zao, au kuyaacha macho ya wajane yadhoofike, [17] kama nimekula chakula changu mwenyewe, bila kuwashirikisha yatima; [18] lakini tangu ujana wangu nimemlea yatima kama ambavyo baba angefanya, nami tangu kuzaliwa kwangu nimewaongoza wajane: [19] kama nilimwona yeyote akiteseka kwa kukosa nguo, au mtu mhitaji asiye na mavazi [20] ambaye wala moyo wake haukunibariki kwa kumpatia joto kwa mavazi ya manyoya ya kondoo zangu, [21] na kama nimeinua mkono wangu dhidi ya yatima, nikijua kuwa nina ushawishi mahakamani, [22] basi mkono wangu na unyofoke toka begani mwangu, nao na uvunjike kutoka kiungio chake. [23] Kwa kuwa niliogopa uharibifu kutoka kwa Mungu, nami kwa kuuogopa utukufu wake sikuweza kufanya mambo kama hayo. [24] “Kama nimeweka tumaini langu kwenye dhahabu, au kuiambia dhahabu safi, ‘Wewe ndiwe salama yangu,’ [25] kama nimefurahia wingi wa utajiri wangu, ustawi ambao mikono yangu ilikuwa imepata, [26] kama nimelitazama jua katika kungʼaa kwake au mwezi ukienda kwa fahari yake, [27] hivyo moyo wangu kushawishiwa kwa siri, au kubusu mkono wangu kwa kuviheshimu, [28] basi hiyo pia ingekuwa dhambi ya kuhukumiwa, kwa kuwa ningekuwa si mwaminifu kwa Mungu aishiye juu sana. [29] “Kama nimeshangilia msiba wa adui yangu, au kutazama kwa furaha taabu iliyomjia, [30] lakini sikuruhusu kinywa changu kufanya dhambi kwa kuomba laana dhidi ya maisha yake; [31] kama watu wa nyumbani mwangu kamwe hawakusema, ‘Ni nani ambaye hajashibishwa na nyama ya Ayubu?’ [32] Lakini hakuna mgeni aliyelala njiani, kwa maana mlango wangu ulikuwa wazi kwa msafiri; [33] kama nimeifunika dhambi yangu kama wanadamu wengine wafanyavyo, kwa kuficha hatia yangu moyoni mwangu, [34] kwa sababu ya kuogopa umati wa watu, na hivyo kuwa na hofu ya kudharauliwa na jamaa, nikanyamaza kimya nisitoke nje ya mlango: [35] (“Laiti kama angekuwepo mtu wa kunisikia! Tazama sasa ninatia sahihi kwenye utetezi wangu: Mwenyezi na anijibu; mshtaki wangu na aweke mashtaka yake kwenye maandishi. [36] Hakika ningeyavaa begani mwangu, ningeyavaa kama taji. [37] Ningempa hesabu ya kila hatua yangu, ningemwendea kama mwana wa mfalme.) [38] “Kama nchi yangu inalia dhidi yangu, na mifereji yake yote imelowana kwa machozi, [39] kama nimekula mazao yake bila malipo, au kuvunja mioyo ya wapangaji wake, [40] basi miiba na iote badala ya ngano, na magugu badala ya shayiri.” Mwisho wa maneno ya Ayubu.
