Ayubu 30:1-31 ONEN
[1] “Lakini sasa watu wadogo kwa umri kuniliko wananidhihaki, watu ambao baba zao ningekataa kwa dharau kuwaweka pamoja na mbwa wangu wa kulinda kondoo. [2] Nguvu za mikono yao zingekuwa na faida gani kwangu, kwa kuwa nguvu zao zilikuwa zimewaishia? [3] Wakiwa wamekonda kutokana na kupungukiwa na kwa njaa, walizurura usiku katika nchi kame iliyo ukiwa. [4] Katika vichaka walikusanya mimea ya chumvi, nacho chakula chao kilikuwa mizizi ya mti wa mfagio. [5] Walifukuzwa mbali na watu wao, wakipigiwa kelele kama wevi. [6] Walilazimika kuishi katika mikondo ya vijito vilivyokauka, kwenye majabali na mahandaki. [7] Kwenye vichaka walilia kama punda, na walijisongasonga pamoja kwenye vichaka. [8] Wao ni watoto wa wapumbavu wenye asili ya ubaya, waliofukuzwa watoke katika nchi. [9] “Nao sasa wana wao wananidhihaki katika nyimbo; nimekuwa kitu cha dhihaka kwao. [10] Wananichukia sana na kujitenga nami, wala hawasiti kunitemea mate usoni. [11] Sasa kwa kuwa Mungu ameilegeza kamba ya upinde wangu na kunitesa, wamekuwa huru kunitendea waonavyo. [12] Kuume kwangu kundi linashambulia; wao huitegea miguu yangu tanzi, na kunizingira. [13] Huizuia njia yangu, nao hufanikiwa katika kuniletea maafa, nami sina yeyote wa kunisaidia. [14] Wananijia kama watu wapitao katika ufa mpana; katikati ya magofu huja na kunishambulia. [15] Vitisho vimenifunika; heshima yangu imetoweshwa kama kwa upepo, salama yangu imetoweka kama wingu. [16] “Sasa maisha yangu yamefikia mwisho; siku za mateso zimenikamata. [17] Usiku mifupa yangu inachoma; maumivu yanayonitafuna hayatulii kamwe. [18] Kwa uwezo wake mkuu Mungu huwa kwangu kama nguo; hushikamana nami kama ukosi wa vazi langu. [19] Yeye amenitupa kwenye matope, nami nimekuwa kama mavumbi na majivu. [20] “Ee BWANA, ninakulilia wewe lakini hunijibu; ninasimama, nawe unanitazama tu. [21] Wewe unanigeukia bila huruma; unanishambulia kwa nguvu za mkono wako. [22] Unaninyakua na kunipeperusha kwa upepo; umenirusha huku na huko kwenye dhoruba kali. [23] Ninajua utanileta mpaka kifoni, mahali ambapo wenye uhai wote wamewekewa. [24] “Hakika hakuna yeyote amshambuliaye mhitaji, anapoomba msaada katika shida yake. [25] Je, sikulia kwa ajili ya wale waliokuwa katika taabu? Je, nafsi yangu haikusononeka kwa ajili ya maskini? [26] Lakini nilipotazamia mema, mabaya yalinijia; nilipotafuta nuru, ndipo giza lilipokuja. [27] Kusukwasukwa ndani yangu kamwe hakutulii; siku za mateso zinanikabili. [28] Ninazunguka nikiwa nimeungua, lakini si kwa jua; ninasimama katika kusanyiko nikiomba msaada. [29] Nimekuwa ndugu wa mbweha, rafiki wa mabundi. [30] Ngozi yangu imekuwa nyeusi nayo inachunika; mifupa yangu inaungua kwa homa. [31] Kinubi changu kimegeuka kuwa maombolezo, nayo filimbi yangu imekuwa sauti ya kilio.
