[1] Ayubu akaendelea na hoja yake, akasema: [2] “Tazama jinsi ninavyoitamani miezi iliyopita, zile siku ambazo Mungu alikuwa akinilinda, [3] wakati taa yake iliniangazia kichwani changu, na kwa mwanga wake Mungu nikapita katikati ya giza! [4] Natamani siku zile nilizokuwa katika ustawi wangu, wakati urafiki wa Mungu wa ndani ulipoibariki nyumba yangu, [5] wakati Mwenyezi alikuwa pamoja nami, nao watoto wangu walikuwa wamenizunguka, [6] wakati njia yangu ilikuwa imenyweshewa siagi, nao mwamba ukanimiminia vijito vya mafuta ya zeituni. [7] “Wakati nilipokwenda kwenye lango la mji na kuketi katika kiwanja, [8] vijana waliniona wakakaa kando, nao wazee walioketi wakasimama; [9] wakuu wakaacha kuzungumza na kuziba vinywa vyao kwa mikono yao; [10] wenye vyeo wakanyamazishwa, nazo ndimi zao zikagandamana na makaakaa ya vinywa vyao. [11] Yeyote aliyenisikia alinena mema juu yangu, nao walioniona walinisifu, [12] kwa sababu nilimwokoa maskini aliyeomba msaada, naye yatima aliyekuwa hana wa kumsaidia. [13] Mtu aliyekuwa karibu kufa alinibariki, nami niliufanya moyo wa mjane kuimba. [14] Niliivaa haki kama vazi langu; uadilifu ulikuwa joho langu na kilemba changu. [15] Nilikuwa macho ya kipofu na miguu kwa kiwete. [16] Nilikuwa baba kwa mhitaji; nilimtetea mgeni. [17] Niliyavunja meno makali ya waovu, na kuwapokonya wahanga kwenye meno yao. [18] “Nikafikiri, ‘Nitafia katika nyumba yangu mwenyewe, nazo siku zangu zitakuwa nyingi kama chembechembe za mchanga. [19] Mizizi yangu itafika mpaka kwenye maji, nao umande utakaa juu ya matawi yangu usiku kucha. [20] Utukufu wangu utabakia kuwa mpya ndani yangu, upinde wangu daima utaendelea kuwa mpya mkononi mwangu.’ [21] “Watu walinisikiliza kwa tumaini, wakingojea ushauri wangu kwa utulivu. [22] Baada ya mimi kuzungumza, hawakusema zaidi; maneno yangu yaliingia masikioni mwao kwa makini. [23] Waliningojea kama manyunyu ya mvua na kuyapokea maneno yangu kama ardhi inyonyavyo mvua ya vuli. [24] Walipokata tamaa niliwaonyesha uso wa furaha; nuru ya uso wangu ilikuwa ya thamani kwao. [25] Niliwachagulia njia na kukaa kama mkuu wao; niliishi kama mfalme katikati ya majeshi yake; nikawa kama yeye anayewafariji waombolezaji.