Ayubu 28:1-28 ONEN

[1] “Kuna machimbo ya fedha, na mahali dhahabu isafishwapo. [2] Chuma hupatikana ardhini, nayo shaba huyeyushwa kutoka mawe ya madini. [3] Mwanadamu hukomesha giza; huyatafuta hadi sehemu iliyo mbali, kwa ajili ya kuchimbua mawe yenye madini katika giza jeusi sana. [4] Huchimba shimo jembamba mbali na makao ya watu, mahali paliposahaulika na nyayo za wanadamu; mbali na wanadamu huningʼinia na kupembea kwa kamba. [5] Ardhi, ambako chakula hutoka, chini hugeuzwa kwa moto; [6] yakuti samawi hutoka katika miamba yake, nalo vumbi lake lina vipande vya dhahabu. [7] Hakuna ndege awindaye aijuaye njia ile iliyofichika, wala hakuna jicho la mwewe lililoiona. [8] Wanyama wa porini wanaotamba hawajawahi kupakanyaga, wala simba azungukaye huko. [9] Mikono ya mwanadamu hushambulia miamba migumu sana, na kuiacha wazi mizizi ya milima. [10] Hutoboa shimo refu la kupenya chini kwa chini kwenye miamba; macho yake huona hazina zake zote. [11] Hutafuta vyanzo vya mito na kuvileta vitu vilivyofichika katika nuru. [12] “Lakini hekima inaweza kupatikana wapi? Ufahamu unakaa wapi? [13] Mwanadamu hatambui thamani yake; haiwezi kupatikana katika nchi ya walio hai. [14] Kilindi husema, ‘Haiko ndani yangu’; bahari nayo husema, ‘Haiko pamoja nami.’ [15] Haiwezi kununuliwa kwa dhahabu safi kuliko zote, wala thamani yake haiwezi kupimwa kwa fedha. [16] Haiwezi kununuliwa kwa dhahabu ya Ofiri, kwa shohamu ya thamani kubwa au yakuti samawi ya thamani kubwa. [17] Dhahabu wala mawe maangavu haviwezi kulinganishwa nayo, wala haiwezi hubadilishwa na vito vya dhahabu. [18] Marijani na yaspi hazistahili kutajwa; thamani ya hekima ni zaidi ya akiki nyekundu. [19] Yakuti manjano ipatikanayo Kushi haiwezi kulinganishwa nayo, wala haiwezi kununuliwa kwa dhahabu safi. [20] “Ni wapi basi hekima itokako? Ufahamu hukaa wapi? [21] Imefichika machoni pa kila kitu kilicho hai, imesitiriwa hata kwa ndege wa angani. [22] Uharibifu na Mauti husema, ‘Ni uvumi wake tu uliotufikia masikioni mwetu.’ [23] Mungu anaifahamu njia ya kuiendea hekima na ndiye peke yake anayefahamu inakokaa, [24] kwa maana yeye huitazama miisho ya dunia na huona kila kitu chini ya mbingu. [25] Alipofanyiza nguvu za upepo na kuyapima maji, [26] alipofanya maagizo kwa ajili ya mvua na njia kwa ajili ya umeme wa radi, [27] ndipo alipoitazama hekima na kuikadiria thamani yake, akaithibitisha na kuihakikisha. [28] Naye Mungu akamwambia mwanadamu, ‘Kumcha BWANA: hiyo ndiyo hekima, nako kujitenga na uovu ndio ufahamu.’ ”

About this translation

Life Bible app icon
Get the Life Bible app Read offline, sync highlights and notes, and study with your library on any device.