[1] Ndipo Ayubu akaendelea na hoja yake, akasema: [2] “Hakika kama Mungu aishivyo, aliyeninyima haki yangu, Mwenyezi ambaye amenifanya nionje uchungu wa nafsi, [3] kwa muda wote nitakaokuwa na uhai ndani yangu, nayo pumzi ya Mungu ikiwa puani mwangu, [4] midomo yangu haitanena uovu, wala ulimi wangu hautatamka udanganyifu. [5] Sitakubaliana nanyi kabisa kuwa mko sahihi; hadi nife, sitakana uadilifu wangu. [6] Nitadumisha haki yangu wala sitaiacha; dhamiri yangu haitanisuta muda wote ninaoishi. [7] “Watesi wangu wawe kama waovu, nao adui zangu wawe kama wasio haki! [8] Kwa maana mtu asiyemcha Mungu analo tegemeo gani anapokatiliwa mbali, Mungu anapouondoa uhai wake? [9] Je, Mungu husikiliza kilio chake, shida zimjiapo? [10] Je, anaweza kumfurahia Mwenyezi? Je, atamwita Mungu nyakati zote? [11] “Nitawafundisha juu ya uweza wa Mungu; njia za Mwenyezi sitazificha. [12] Ninyi nyote mmeona hili wenyewe. Ni ya nini basi mazungumzo haya yasiyo na maana? [13] “Hili ndilo fungu ambalo Mungu humpa mtu mwovu, urithi ule mtu mdhalimu anapokea kutoka kwa Mwenyezi: [14] Hata kama watoto wake watakuwa wengi kiasi gani, fungu lao ni kuuawa kwa upanga; wazao wake hawatakuwa kamwe na chakula cha kuwatosha. [15] Tauni itawazika wale watakaonusurika miongoni mwao, nao wajane wao hawatawaombolezea. [16] Ajapokusanya fedha nyingi kama mavumbi, na mavazi kama malundo ya udongo wa mfinyanzi, [17] yale yote mtu mwovu aliyojiwekea akiba, mwenye haki atayavaa, naye asiye na hatia ataigawanya fedha yake. [18] Nyumba aijengayo ni kama utando wa buibui, kama kibanda alichotengeneza mlinzi. [19] Yeye hulala akiwa tajiri, lakini ndiyo mara ya mwisho; afunguapo macho yake, yote yametoweka. [20] Vitisho humjia kama mafuriko; dhoruba humkumba ghafula usiku. [21] Upepo mkali wa mashariki humchukua, naye hutoweka; humzoa kutoka mahali pake. [22] Humvurumisha bila huruma, huku akikimbia kasi kukwepa nguvu zake. [23] Upepo humpigia makofi kwa dharau, na kumfukuza atoke mahali pake.