[1] Kisha Ayubu akajibu: [2] “Tazama jinsi ulivyomsaidia mtu asiye na uwezo! Jinsi ulivyouokoa mkono ulio dhaifu! [3] Ni shauri gani ulilompa yeye asiye na hekima? Nayo ni busara gani kubwa uliyoonyesha! [4] Ni nani aliyekusaidia kutamka maneno hayo? Nayo ni roho ya nani iliyosema kutoka kinywani mwako? [5] “Wafu wako katika maumivu makuu, wale walio chini ya maji na wale waishio ndani yake. [6] Mauti iko wazi mbele za Mungu; Uharibifu haukufunikwa. [7] Hutandaza anga la kaskazini mahali patupu; naye huiningʼiniza dunia mahali pasipo na kitu. [8] Huyafungia maji kwenye mawingu yake, hata hivyo mawingu hayapasuki kwa uzito wake. [9] Huufunika uso wa mwezi mpevu, akitandaza mawingu juu yake. [10] Amechora mstari wa upeo juu ya uso wa maji, ameweka mpaka wa nuru na giza. [11] Nguzo za mbingu nazo zatetemeka, zinatishika anapozikemea. [12] Kwa nguvu zake aliisukasuka bahari; kwa hekima yake alimkata Rahabu vipande vipande. [13] Aliisafisha anga kwa pumzi yake; kwa mkono wake alimchoma joka aendaye mbio. [14] Haya ni mambo madogo tu katika matendo yake; tazama jinsi ulivyo mdogo mnongʼono tunaousikia kumhusu! Ni nani basi awezaye kuelewa ngurumo za nguvu zake?”