[1] Ndipo Ayubu akajibu: [2] “Hata leo malalamiko yangu ni chungu; mkono wake ni mzito juu yangu hata nikiugua. [3] Laiti ningefahamu mahali pa kumwona; laiti ningeweza kwenda mahali akaapo! [4] Ningeliweka shauri langu mbele zake, na kukijaza kinywa changu na hoja. [5] Ningejua kwamba angenijibu nini, na kuelewa lile ambalo angelisema. [6] Je, angenipinga kwa nguvu nyingi? La, asingenigandamiza. [7] Hapo mtu mwadilifu angeweka shauri lake mbele zake, nami ningeokolewa milele na mhukumu wangu. [8] “Lakini nikienda mashariki, hayupo; nikienda magharibi, simpati. [9] Anapokuwa kazini pande za kaskazini, simwoni; akigeukia kusini, nako simwoni hata kidogo. [10] Lakini anaijua njia niiendeayo; akiisha kunijaribu, nitatoka kama dhahabu. [11] Nyayo zangu zimefuata hatua zake kwa karibu; nimeishika njia yake bila kukengeuka. [12] Sijaziacha amri zilizotoka midomoni mwake; nimeyathamini maneno ya kinywa chake kuliko chakula changu cha kila siku. [13] “Lakini yeye husimama peke yake; ni nani awezaye kumpinga? Yeye hufanya lolote atakalo. [14] Hutimiliza maagizo yake dhidi yangu, na bado anayo mipango mingi kama hiyo ambayo ameiweka akiba. [15] Hiyo ndiyo sababu ninaingiwa na hofu mbele zake; nifikiriapo haya yote ninamwogopa. [16] Mungu ameufanya moyo wangu kuzimia; yeye Mwenyezi amenitia hofu. [17] Hata hivyo sijanyamazishwa na giza, wala kwa giza nene linalofunika uso wangu.