Ayubu 24:1-25 ONEN
[1] “Kwa nini Mwenyezi asiweke nyakati kwa ajili ya hukumu? Kwa nini wale wamjuao wazitafute siku kama hizo bila mafanikio? [2] Watu husogeza mawe ya mpaka; huchunga makundi ya wanyama waliyonyangʼanya kwa nguvu. [3] Huwanyangʼanya yatima punda wao, na kumchukua rehani fahali wa mjane. [4] Humsukuma mhitaji kutoka njia, na kuwafanya maskini wote wa nchi kulazimika kujificha. [5] Kama punda-mwitu jangwani, maskini huzunguka katika kazi zao za kutafuta chakula; mahali palipo jangwa huwapa chakula cha watoto wao. [6] Hukusanya chakula mashambani na kuokota masazo katika mashamba ya mizabibu ya waovu. [7] Kwa kukosa nguo, usiku kucha hukaa uchi; hawana chochote cha kujifunika baridi. [8] Hutota kwa mvua za mlimani, nao huikumbatia miamba kwa ajili ya kukosa pa kujisitiri. [9] Mtoto yatima hupokonywa matitini; mtoto wachanga wa maskini hunyakuliwa kwa ajili ya deni. [10] Kwa kukosa nguo, hutembea uchi; hubeba miganda ya ngano, lakini huwa na njaa. [11] Hukamua zeituni katika mawe ya kusagia; hukanyaga mashinikizo, lakini wanaona kiu. [12] Kilio cha huzuni cha wanaokufa kinapaa kutoka mjini, nazo nafsi za waliojeruhiwa zinalilia msaada. Lakini Mungu hamlaumu mtu yeyote kwa kutenda mabaya. [13] “Wako wale wanaoiasi nuru, wasiofahamu njia zake wala hawakai katika mapito yake. [14] Wakati mwanga wa mchana unapotoweka, muuaji huinuka naye huwaua maskini na mhitaji; wakati wa usiku hunyemelea kama mwizi. [15] Jicho la mzinzi hungojea wakati wa giza, naye hufikiri, ‘Hakuna jicho litakaloniona,’ naye huuficha uso wake. [16] Katika giza, huvunja majumba, lakini wakati wa mchana hujifungia ndani; hawataki kufanya lolote nuruni. [17] Kwa wote hawa, giza nene ndiyo asubuhi yao; hujifanya rafiki na vitisho vya gizani. [18] “Lakini wao ni povu juu ya maji; sehemu yao juu ya nchi imelaaniwa, hivyo hakuna hata mmoja aendaye kwenye shamba la mizabibu. [19] Kama vile joto na hari vinyakuavyo theluji iliyoyeyuka, ndivyo kuzimu kuwanyakuavyo waliotenda dhambi. [20] Tumbo lililowazaa huwasahau, nao huwa karamu ya mabuu; watu waovu hawakumbukwi tena, lakini huvunjika kama mti. [21] Huwafanya mawindo wanawake tasa na wasio na watoto, nao hawaonyeshi huruma kwa wajane. [22] Lakini Mungu huwakokota wenye nguvu kwa uwezo wake; ingawa wamestawi, hawana hakika ya maisha. [23] Aweza akawaacha wakapumzika wakijihisi salama, lakini macho yake yanaona njia zao. [24] Kwa kitambo kidogo hutukuka, hatimaye hutoweka; hushushwa na kukusanywa kama wengine wote, hukatwa kama masuke ya nafaka. [25] “Kama hili sivyo, ni nani awezaye kunithibitisha kuwa mwongo, na kuyafanya maneno yangu kuwa si kitu?”
