Ayubu 22:1-30 ONEN
[1] Ndipo Elifazi Mtemani akajibu: [2] “Je, mwanadamu aweza kuwa wa faida kwa Mungu? Je, hata mtu mwenye hekima aweza kumfaidi? [3] Je, Mwenyezi angefurahia nini kama ungekuwa mwadilifu? Au je, yeye angepata faida gani kama njia zako zingekuwa kamilifu? [4] “Je, ni kwa ajili ya utaua wako ndiyo maana anakukemea na kuleta mashtaka dhidi yako? [5] Je, uovu wako si mkuu? Dhambi zako si hazina mwisho? [6] Umedai dhamana kwa ndugu zako bila sababu; umewavua watu nguo zao, ukawaacha uchi. [7] Hukumpa maji aliyechoka, nawe ulimnyima chakula mwenye njaa, [8] ingawa ulikuwa mtu mwenye uwezo ukimiliki nchi: mtu uliyeheshimiwa, ukiishi ndani yake. [9] Umewafukuza wajane mikono mitupu na kuzivunja nguvu za yatima. [10] Ndiyo sababu mitego imekuzunguka pande zote, hatari ya ghafula inakutia hofu, [11] ndiyo sababu ni giza sana huwezi kuona, tena ndiyo sababu mafuriko ya maji yamekufunika. [12] “Je, Mungu hayuko katika mbingu za juu? Juu kuliko nyota zilizo juu sana! [13] Hivyo wewe wasema, ‘Mungu anajua nini?’ Je, yeye huhukumu katika giza kama hilo? [14] Mawingu mazito ni pazia lake, hivyo hatuoni sisi atembeapo juu ya anga la dunia. [15] Je, utaifuata njia ya zamani, ambayo watu waovu waliikanyaga? [16] Waliondolewa kabla ya wakati wao, misingi yao ikachukuliwa na mafuriko. [17] Walimwambia Mungu, ‘Tuache sisi! Huyo Mwenyezi aweza kutufanyia nini?’ [18] Lakini ndiye alizijaza nyumba zao na vitu vizuri, hivyo ninajitenga mbali na mashauri ya waovu. [19] “Wenye haki wanaona maangamizi yao na kufurahi, nao wasio na hatia huwadhihaki, wakisema, [20] ‘Hakika adui zetu wameangamizwa, nao moto umeteketeza mali zao.’ [21] “Mjue sana Mungu ili uwe na amani, ndipo mema yatakapokujia. [22] Uyapokee mafundisho toka kinywani mwake, na maneno yake uyaweke moyoni mwako. [23] Kama ukimrudia Mwenyezi, utarudishwa upya: Kama ukiuondoa uovu uwe mbali na hema lako, [24] kama dhahabu yako ukiihesabu kama mavumbi, dhahabu yako ya Ofiri kama miamba ya mabondeni, [25] ndipo Mwenyezi atakuwa dhahabu yako, naye atakuwa fedha yako iliyo bora. [26] Hakika ndipo utakapojifurahisha kwa Mwenyezi, nawe utamwinulia Mungu uso wako. [27] Utamwomba yeye, naye atakusikia, nawe utazitimiza nadhiri zako. [28] Utakusudia jambo nalo litatendeka, nao mwanga utaangazia njia zako. [29] Watu watakaposhushwa, nawe ukasema, ‘Wainue!’ ndipo atamwokoa aliyevunjika moyo. [30] Atamwokoa hata yule ambaye ana hatia, ataokolewa kwa sababu ya usafi wa mikono yako.”
