Ayubu 21:1-34 ONEN
[1] Ndipo Ayubu akajibu: [2] “Yasikilizeni maneno yangu kwa makini; hii na iwe faraja mnayonipa mimi. [3] Nivumilieni ninapozungumza, nami nikishazungumza, endeleeni kunidhihaki. [4] “Je, kwani malalamiko yangu yanaelekezwa kwa mwanadamu? Kwa nini nisikose subira? [5] Niangalieni mkastaajabu; mkaweke mkono juu ya vinywa vyenu. [6] Ninapowaza juu ya hili, ninaogopa, nao mwili wangu unatetemeka. [7] Kwa nini waovu wanaendelea kuishi, wakifikia umri wa uzee na kuendelea kuwa na nguvu? [8] Huwaona watoto wao wakithibitika wakiwa wamewazunguka, wazao wao mbele za macho yao. [9] Nyumba zao zi salama wala hakuna hofu; fimbo ya Mungu haiko juu yao. [10] Madume yao ya ngʼombe huvyaza bila kushindwa kamwe; ngʼombe wao huzaa wala hawaharibu mimba. [11] Huwatoa watoto wao nje kama kundi; wadogo wao huchezacheza. [12] Huimba nyimbo kwa matari na kwa kinubi, nao huifurahia sauti ya filimbi. [13] Huitumia miaka yao katika mafanikio nao hushuka kaburini kwa amani. [14] Lakini humwambia Mungu, ‘Tuache sisi!’ Hatuna haja ya kufahamu njia zako. [15] Mwenyezi ni nani hata tumtumikie? Tutapata faida gani kumwomba? [16] Lakini kufanikiwa kwao hakupo mikononi mwao wenyewe, hivyo najitenga mbali na shauri la waovu. [17] “Lakini ni mara ngapi taa ya waovu huzimwa? Ni mara ngapi maafa huwajia, yale yawapatayo ambayo Mungu huwapangia katika hasira yake? [18] Ni mara ngapi huwa kama majani makavu mbele ya upepo, kama makapi yachukuliwayo na dhoruba? [19] Imesemekana, ‘Mungu huiweka akiba adhabu ya mtu kwa ajili ya wanawe.’ Mungu na amlipe mtu mwenyewe, ili apate kulijua! [20] Macho yake mwenyewe na yaone maangamizi yake; yeye na ainywe ghadhabu ya Mwenyezi. [21] Kwani anajali nini kuhusu jamaa anayoiacha nyuma, miezi yake aliyopangiwa ifikapo mwisho? [22] “Je, yuko mtu yeyote awezaye kumfundisha Mungu maarifa, iwapo yeye ndiye ahukumuye hata walio juu ya wote? [23] Mtu mmoja hufa akiwa na nguvu zake kamili, akiwa salama na mwenye raha kamili, [24] mwili wake ukiwa umenawiri, nayo mifupa yake ikiwa imejaa mafuta ndani yake. [25] Mtu mwingine hufa katika uchungu wa nafsi, akiwa hajafurahia kamwe jambo lolote zuri. [26] Hao wote hulala mavumbini, nao mabuu huwafunika wote. [27] “Ninayajua kikamilifu yale mnayoyafikiri, mipango ambayo kwayo mngenitendea mabaya. [28] Mwasema, ‘Iko wapi sasa nyumba ya huyo mtu mkuu, mahema ambayo watu waovu walikaa?’ [29] Je, hamkuwahi kuwauliza hao wanaosafiri? Je, hamkutafakari taarifa zao: [30] kwamba mtu mwovu huepushwa kutoka siku ya maafa, kwamba huokolewa kutoka siku ya ghadhabu? [31] Ni nani hulaumu matendo yake mbele ya uso wake? Ni nani ampatilizaye kwa yale aliyoyatenda? [32] Hupelekwa kaburini, nao ulinzi ukawekwa kwenye kaburi lake. [33] Udongo ulio bondeni ni mtamu kwake; watu wote watamfuata, nao umati wa watu usiohesabika umemtangulia. [34] “Hivyo ninyi mnawezaje kunifariji kwa upuzi wenu? Hakuna kilichosalia cha majibu yenu isipokuwa uongo!”
