Ayubu 20:1-29 ONEN
[1] Ndipo Sofari Mnaamathi akajibu: [2] “Mawazo yanayonisumbua yananisukuma kujibu, kwa sababu nimehangaika sana. [3] Ninasikia makaripio ambayo yananivunjia heshima, nao ufahamu wangu unanisukuma kujibu. [4] “Hakika unajua jinsi ilivyokuwa tangu zamani, tangu zamani mwanadamu alipowekwa duniani, [5] macheko ya mtu mwovu ni ya muda mfupi, nayo furaha ya wasiomcha Mungu hudumu kwa kitambo tu. [6] Ingawa kujikweza kwake hufikia mbinguni na kichwa chake hugusa mawingu, [7] ataangamia milele kama mavi yake mwenyewe. Wale waliomwona watauliza, ‘Yuko wapi?’ [8] Kama ndoto hutoweka, wala hapatikani tena, amefukuziwa mbali kama maono ya usiku. [9] Jicho lililomwona halitamwona tena; mahali pake hapatamwona tena. [10] Watoto wake watalipa yote baba yao aliyowadhulumu maskini, nayo mikono yake itarudisha mali yote aliyonyangʼanya watu. [11] Nguvu za ujana zilizoijaza mifupa yake, zitalala naye mavumbini. [12] “Ingawa uovu ni mtamu kinywani mwake naye huuficha chini ya ulimi wake, [13] ingawa hawezi kukubali kuuachia uende, lakini huuweka kinywani mwake. [14] Hata hivyo chakula chake kitakuwa kichungu tumboni mwake, nacho kitakuwa sumu kali ya nyoka ndani yake. [15] Atatema mali alizozimeza; Mungu atalifanya tumbo lake kuzitapika. [16] Atanyonya sumu za majoka; meno ya nyoka mwenye sumu kali yatamuua. [17] Hatafurahia vijito, mito inayotiririsha asali na siagi. [18] Vile alivyovitaabikia atavirudisha bila kuvila; hatafurahia faida itokanayo na biashara yake. [19] Kwa kuwa aliwaonea maskini na kuwaacha pasipo kitu; amenyangʼanya kwa nguvu nyumba asizozijenga. [20] “Hakika hatakuwa na raha katika kutamani kwake sana; hawezi kujiokoa mwenyewe kwa hazina zake. [21] Hakuna chochote kitakachosalia kwa ajili yake ili ale; kufanikiwa kwake hakutadumu. [22] Katikati ya wingi wa ustawi wake, dhiki itampata; taabu itamjia kwa nguvu zote. [23] Atakapokuwa amelijaza tumbo lake, Mungu ataionyesha ghadhabu kali dhidi yake, na kumnyeshea mapigo juu yake. [24] Ijapokuwa aikimbia silaha ya chuma, mshale wa shaba utamchoma. [25] Atauchomoa katika mgongo wake, ncha ingʼaayo kutoka ini lake. Vitisho vitakuja juu yake; [26] giza nene linavizia hazina zake. Moto usiopepewa na mtu utamteketeza, na kuangamiza yaliyosalia nyumbani mwake. [27] Mbingu zitaweka wazi hatia yake, nayo nchi itainuka kinyume chake. [28] Mafuriko yataichukua nyumba yake, maji yaendayo kasi katika siku ya ghadhabu ya Mungu. [29] Hili ndilo fungu Mungu alilowagawia waovu, urithi uliowekwa kwa ajili yao na Mungu.”
