[1] Ndipo Ayubu akajibu: [2] “Je, mtaendelea kunitesa mpaka lini, na kuniponda kwa maneno yenu? [3] Mara kumi hizi mmenishutumu; bila aibu mnanishambulia. [4] Kama ni kweli nimepotoka, kosa langu ninabaki kuhusika nalo mwenyewe. [5] Kama kweli mngejitukuza wenyewe juu yangu, na kutumia unyonge wangu dhidi yangu, [6] basi jueni kuwa Mungu amenitendea yaliyo mabaya, naye amekokota wavu wake kunizunguka. [7] “Ingawa ninalia, ‘Nimetendewa mabaya!’ sipati jibu; ingawa ninaomba msaada, hakuna haki. [8] Yeye ameizuia njia yangu hivyo siwezi kupita; ameyafunika mapito yangu na giza. [9] Amenivua heshima yangu, na kuniondolea taji kichwani pangu. [10] Amenibomoa kila upande hadi nimeisha; amelingʼoa tegemeo langu kama mti. [11] Hasira yake imewaka juu yangu; amenihesabu kuwa miongoni mwa adui zake. [12] Majeshi yake yananisogelea kwa nguvu; yamenizingira, yamepiga kambi kulizunguka hema langu. [13] “Amewatenga ndugu zangu mbali nami; wale tunaojuana nao wamefarakana nami kabisa. [14] Watu wa jamaa yangu wamekwenda mbali; rafiki zangu wamenisahau. [15] Wageni wangu na watumishi wangu wa kike wananiona kama mgeni; wananitazama kama mgeni. [16] Namwita mtumishi wangu, wala haitiki, ingawa namwomba kwa kinywa changu mwenyewe. [17] Pumzi ya kinywa changu ni kinyaa kwa mke wangu; nimekuwa chukizo mno kwa ndugu zangu mwenyewe. [18] Hata watoto wadogo hunidhihaki; ninapojitokeza, hunifanyia mzaha. [19] Rafiki zangu wa moyoni wote wananichukia kabisa; wale niwapendao wamekuwa kinyume nami. [20] Mimi nimebaki mifupa na ngozi tu; nimeponea nikiwa karibu kufa. [21] “Nihurumieni, rafiki zangu, kuweni na huruma, kwa kuwa mkono wa Mungu umenipiga. [22] Kwa nini mnanifuatia kama Mungu afanyavyo? Hamtosheki kamwe na mwili wangu? [23] “Laiti maneno yangu yangewekwa kwenye kumbukumbu, laiti kwamba yangeandikwa kwenye kitabu, [24] kwamba yangechorwa kwenye risasi kwa kifaa cha chuma, au kuyachonga juu ya mwamba milele! [25] Ninajua kwamba Mkombozi wangu yu hai, naye kwamba mwishoni atasimama juu ya nchi. [26] Nami baada ya ngozi yangu kuharibiwa, bado nikiwa na mwili huu nitamwona Mungu; [27] mimi nitamwona kwa macho yangu mwenyewe: mimi, wala si mwingine. Tazama jinsi moyo wangu unavyomtamani sana! [28] “Kama mkisema, ‘Tazama tutakavyomwinda, maadamu mzizi wa tatizo uko ndani yake,’ [29] ninyi wenyewe uogopeni upanga, kwa kuwa ghadhabu italeta adhabu kwa upanga, nanyi ndipo mtakapojua kwamba kuna hukumu.”