[1] Bildadi Mshuhi akajibu: [2] “Je, ni lini utafika mwisho wa maneno haya? Uwe mwenye busara, nasi ndipo tutakapoweza kuongea. [3] Kwa nini sisi tunafikiriwa kama wanyama, na kuonekana wajinga machoni pako? [4] Wewe unayejirarua mwenyewe vipande vipande katika hasira yako, je, dunia iachwe kwa ajili yako wewe? Au ni lazima miamba iondolewe mahali pake? [5] “Taa ya mwovu imezimwa, nao mwali wa moto wake umezimika. [6] Mwanga hemani mwake umekuwa giza; taa iliyo karibu naye imezimika. [7] Nguvu za hatua zake zimedhoofishwa; shauri lake baya litamwangusha. [8] Miguu yake imemsukumia kwenye wavu, naye anatangatanga kwenye matundu ya wavu. [9] Tanzi litamkamata kwenye kisigino; mtego utamshikilia kwa nguvu. [10] Kitanzi kimefichwa ardhini kwa ajili yake; mtego uko kwenye njia yake. [11] Vitisho vimemtia hofu kila upande, na adui zake humwandama kila hatua. [12] Janga linamwonea shauku; maafa yako tayari kwa ajili yake aangukapo. [13] Nayo yatakula sehemu ya ngozi yake; mzaliwa wa kwanza wa mauti atakula maungo yake. [14] Atangʼolewa kutoka usalama wa hema lake, na kupelekwa kwa mfalme wa vitisho. [15] Moto utakaa katika hema lake; moto wa kiberiti utamwagwa juu ya makao yake. [16] Mizizi yake chini itakauka na matawi yake juu yatanyauka. [17] Kumbukumbu lake litatoweka katika dunia, wala hatakuwa na jina katika nchi. [18] Ameondolewa nuruni na kusukumiwa gizani, naye amefukuzwa mbali atoke duniani. [19] Hana mtoto wala mzao miongoni mwa watu wake, wala aliyenusurika mahali alipoishi. [20] Watu wa magharibi watashangaa yaliyompata; watu wa mashariki watapatwa na hofu. [21] Hakika ndivyo yalivyo makao ya mtu mwovu; ndivyo palivyo mahali pake mtu asiyemjua Mungu.”