[1] Moyo wangu umevunjika, siku zangu zimefupishwa, kaburi linaningojea. [2] Hakika wenye mizaha wamenizunguka; macho yangu yamebaki kutazama uadui wao. [3] “Ee Mungu, nipe dhamana unayodai. Ni nani mwingine atakayeweka dhamana kwa ajili yangu? [4] Umezifunga akili zao zisipate ufahamu, kwa hiyo hutawaacha wapate ushindi. [5] Kama mtu akiwashutumu rafiki zake ili apate ujira, macho ya watoto wake yatashindwa kuona. [6] “Mungu amenifanya kitu cha dhihaka kwa kila mtu, mtu ambaye watu humtemea mate usoni. [7] Macho yangu yamefifia kwa ajili ya majonzi; umbile langu lote ni kama kivuli. [8] Watu wanyofu wanatishwa na hili; watu wasio na hatia wanasimama dhidi ya wasiomcha Mungu. [9] Hata hivyo, waadilifu watazishika njia zao, nao wale wenye mikono safi wataendelea kupata nguvu. [10] “Lakini ninyi njooni, ninyi nyote, jaribuni tena! Sitampata mtu mwenye hekima miongoni mwenu. [11] Siku zangu zimepita, mipango yangu imevunjika, vivyo hivyo shauku za moyo wangu. [12] Watu hawa hufanya usiku kuwa mchana, kwenye giza wao husema, ‘Mwanga u karibu.’ [13] Kama nyumba pekee ninayoitarajia ni kaburi, kama nikikitandika kitanda changu gizani, [14] kama nikiuambia uharibifu, ‘Wewe u baba yangu,’ na kuliambia buu, ‘Wewe u mama yangu’ au ‘Dada yangu,’ [15] liko wapi basi tarajio langu? Ni nani awezaye kuona tarajio lolote kwa ajili yangu? [16] Je, litashuka chini hadi kwenye malango ya mauti? Je, tutashuka pamoja mavumbini?”