[1] Kisha Ayubu akajibu: [2] “Nimepata kusikia mambo mengi kama haya, nanyi nyote ni wafariji wenye kutaabisha! [3] Je, maneno yenu mengi yasiyo na maana hayana mwisho? Mna nini hata mwendelee kushindana kwa maneno? [4] Mimi pia ningeweza kuzungumza kama ninyi, kama mngekuwa katika hali yangu; ningeweza kutoa hotuba nzuri dhidi yenu, na kuwatikisia ninyi kichwa changu. [5] Lakini kinywa changu kingewatia moyo; faraja kutoka midomoni mwangu, ingewaletea nafuu. [6] “Lakini kama nikisema, maumivu yangu bado hayatulizwi; nami kama nikijizuia, wala hayaondoki. [7] Ee Mungu, hakika umenichakaza; umewaangamiza kabisa watu wa nyumbani mwangu wote. [8] Umenikunjakunja, nalo limekuwa ushahidi; nako kukonda kwangu kumeongezeka sana na kushuhudia dhidi yangu. [9] Mungu amenishambulia na kunirarua katika hasira yake, na kunisagia meno yake; adui yangu hunikazia macho yake makali. [10] Watu wamenifumbulia vinywa vyao kunidhihaki; hunipiga shavuni mwangu kwa dharau, na kuungana pamoja dhidi yangu. [11] Mungu amenigeuzia kwa watu wabaya, na kunitupa katika makucha ya waovu. [12] Mambo yote yalikuwa mazuri, lakini alinivunjavunja; amenikamata shingo na kuniponda. Amenifanya mimi kuwa shabaha yake; [13] wapiga upinde wake wananizunguka. Bila huruma, huchoma figo zangu, na kuimwaga nyongo yangu juu ya nchi. [14] Huniponda tena na tena; hunishambulia kama shujaa wa vita. [15] “Nimejishonea nguo ya gunia juu ya mwili wangu nami nimekizika kipaji cha uso wangu kwenye vumbi. [16] Uso wangu umekuwa mwekundu kwa kulia, macho yangu yamepigwa na giza kuu. [17] Hata hivyo mikono yangu haijafanya jeuri, na maombi yangu ni safi. [18] “Ee nchi, usiifunike damu yangu, nacho kilio changu kisinyamazishwe kamwe. [19] Hata sasa shahidi wangu yuko mbinguni; wakili wangu yuko juu. [20] Mwombezi wangu ni rafiki yangu macho yangu yamwagapo machozi kwa Mungu; [21] kwa niaba ya mtu anamsihi Mungu kama mtu anavyosihi kwa ajili ya rafiki yake. [22] “Ni miaka michache tu itapita kabla sijaenda safari ambayo sitarudi.