Ayubu 15:1-35 ONEN
[1] Kisha Elifazi Mtemani akajibu: [2] “Je, mtu mwenye hekima hujibu kwa mawazo matupu, au kujaza tumbo lake kwa upepo wenye joto wa mashariki? [3] Je, aweza kubishana juu ya maneno yasiyofaa, kwa hotuba zisizo na maana? [4] Lakini unadhoofisha hata uchaji wa Mungu na kuzuia ibada mbele za Mungu. [5] Dhambi yako inasukuma kinywa chako, nawe umechagua ulimi wa hila. [6] Kinywa chako mwenyewe kinakuhukumu, wala si changu; midomo yako mwenyewe inashuhudia dhidi yako. [7] “Je, wewe ni mtu wa kwanza kuzaliwa? Ulizaliwa kabla ya vilima? [8] Je, wewe husikiliza mashauri ya siri ya Mungu? Je, wewe unaizuia hekima iwe yako mwenyewe? [9] Wewe unajua kitu gani tusichokijua sisi? Unafahamu kitu gani tusichokifahamu sisi? [10] Wale wenye mvi na wazee wako upande wetu, watu ambao ni wazee hata kuliko baba yako. [11] Je, faraja za Mungu hazikutoshi, au maneno yaliyosemwa kwako kwa upole si kitu? [12] Kwa nini moyo wako unakudanganya, na kwa nini macho yako yanangʼaa, [13] ili kwamba upate kutoa hasira yako dhidi ya Mungu, na kumwaga maneno kama hayo kutoka kinywani mwako? [14] “Mwanadamu ni kitu gani, hata aweze kuwa safi, au yeye aliyezaliwa na mwanamke, hata aweze kuwa mwadilifu? [15] Kama Mungu hawaamini watakatifu wake, kama hata mbingu zenyewe si safi machoni pake, [16] sembuse mwanadamu ambaye ni mwovu na mpotovu, ambaye hunywa uovu kama anywavyo maji! [17] “Nisikilize mimi nami nitakueleza, acha nikuambie yale niliyoyaona, [18] ambayo watu wenye hekima wameyanena, bila kuficha lolote walilopokea toka kwa baba zao [19] (wakati ambao wao peke yao ndio walipewa nchi, hakuna mgeni aliyepita miongoni mwao): [20] Mtu mwovu siku zake zote hupata mateso, miaka yote aliwekewa mkorofi. [21] Sauti za kutisha hujaa masikioni mwake; katika kufanikiwa kwake, wanyangʼanyi humshambulia. [22] Hukata tamaa kuokoka gizani; amewekwa kwa ajili ya upanga. [23] Hutangatanga, akitafuta chakula; anajua kwamba siku ya giza iko karibu. [24] Taabu na maumivu makuu vinamtia hofu; humshinda kama mfalme aliye tayari kwa vita, [25] kwa sababu amemkunjia Mungu ngumi yake na kujigamba dhidi ya Mwenyezi, [26] kwa kiburi akishambulia dhidi ya Mungu akiwa na ngao nene, iliyo imara. [27] “Ingawa uso wake umefunikwa na mafuta kwa unene na kiuno chake kimevimba kwa kunenepa, [28] ataishi katika miji ya magofu, na katika nyumba ambazo haziishi mwanadamu yeyote, nyumba zinazokuwa vifusi. [29] Hatatajirika tena, nao utajiri wake hautadumu, wala mali zake hazitakuwa nyingi juu ya nchi. [30] Hatatoka gizani; mwali wa moto utanyausha machipukizi yake, nayo pumzi ya kinywa cha Mungu itamwondolea mbali. [31] Asijidanganye mwenyewe kutumainia ubatili, kwa kuwa hatapata malipo yoyote. [32] Atakuwa amelipwa kikamilifu kabla ya wakati wake, nayo matawi yake hayatastawi. [33] Atafanana na mzabibu uliopukutishwa matunda yake kabla hayajaiva, kama mzeituni unaodondosha maua yake. [34] Kwa kuwa jamii ya wasiomcha Mungu watakuwa tasa, nao moto utateketeza hema za wale wanaopenda rushwa. [35] Hutunga mimba ya madhara na kuzaa uovu; matumbo yao huumba udanganyifu.”
