[1] “Mwanadamu aliyezaliwa na mwanamke siku zake ni chache nazo zimejaa taabu. [2] Huchanua kama ua kisha hunyauka; huwa kama kivuli kipitacho upesi, wala hadumu. [3] Je, unamwekea jicho lako mtu kama huyo? Je, utamleta mbele yako katika hukumu? [4] Ni nani awezaye kutoa kitu safi kutoka kitu najisi? Hakuna awezaye! [5] Siku za mwanadamu zimewekewa mpaka; umekwisha kutangaza idadi ya miezi yake na kuweka mpaka ambao hawezi kuuvuka. [6] Hivyo angalia mbali umwache, hadi awe amekamilisha muda wake kama mtu aliyeajiriwa. [7] “Kwa maana lipo tumaini kwa mti; kama ukikatwa utachipuka tena, nayo machipukizi yake mapya hayatakoma. [8] Mizizi yake yaweza kuchakaa ardhini na kisiki chake kufa udongoni, [9] lakini kwa kupata dalili ya maji utachipua na kutoa machipukizi kama mche. [10] Lakini mwanadamu hufa, na huo ndio mwisho wake; hutoa pumzi ya mwisho, naye hayuko tena! [11] Kama vile maji yatowekavyo katika bahari, au mkondo wa mto ukaushwavyo na kuwa mkavu, [12] ndivyo mwanadamu alalavyo chini asiamke; hadi mbingu zitakapokuwa hazipo tena, wanadamu hawataamka au kuamshwa kutoka kwenye usingizi wao. [13] “Laiti kama ungenificha kaburini, na kunisitiri hadi hasira yako ipite! Laiti ungeniwekea wakati, na kisha ukanikumbuka! [14] Je, kama mtu akifa, aweza kuishi tena? Siku zote za kazi zangu ngumu nitangojea kufanywa upya kwangu. [15] Utaniita nami nitakuitika; utakionea shauku kiumbe ambacho mikono yako ilikiumba. [16] Hakika ndipo utakapozihesabu hatua zangu, lakini hutazifuatia dhambi zangu. [17] Makosa yangu yatafungiwa kwa lakiri kwenye mfuko, nawe utazifunika dhambi zangu. [18] “Lakini kama mlima umomonyokavyo na kufikichika na kama vile mwamba uondolewavyo mahali pake, [19] kama maji yamalizavyo mawe, na mafuriko yachukuavyo udongo, ndivyo unavyoharibu tegemeo la mwanadamu. [20] Humshinda mara moja kwa daima, naye hutoweka; waibadilisha sura yake na kumwondoa. [21] Kama wanawe wakipewa heshima, yeye hafahamu; kama wakidharauliwa, yeye haoni. [22] Yeye hasikii kingine isipokuwa maumivu ya mwili wake mwenyewe, naye huomboleza kwa ajili yake mwenyewe.”