[1] “Macho yangu yameona hili lote, masikio yangu yamesikia na kulielewa. [2] Hayo mnayoyajua mimi pia ninayajua; mimi si mtu duni kuliko ninyi. [3] Lakini ninayo shauku ya kuzungumza na Mwenyezi na kuhojiana shauri langu na Mungu. [4] Ninyi, hata hivyo, hunipakaza uongo; ninyi ni matabibu wasiofaa kitu, ninyi nyote! [5] Laiti wote mngenyamaza kimya! Kwa kuwa kwenu hilo lingekuwa hekima. [6] Sikieni sasa hoja yangu; sikilizeni kusihi kwangu. [7] Je, mtazungumza kwa uovu kwa niaba ya Mungu? Je, mtazungumza kwa udanganyifu kwa niaba yake? [8] Mtamwonyesha upendeleo? Mtamtetea Mungu kwenye mashtaka yake? [9] Je, ingekuwa vyema Mungu akiwahoji ninyi? Je, mngeweza kumdanganya kama ambavyo mngeweza kuwadanganya wanadamu? [10] Hakika angewakemea kama mkiwapendelea watu kwa siri. [11] Je, huo ukuu wake haungewatisha ninyi? Je, hofu yake isingewaangukia ninyi? [12] Maneno yenu ni mithali za majivu; utetezi wenu ni ngome za udongo wa mfinyanzi. [13] “Nyamazeni kimya nipate kusema; kisha na yanipate yatakayonipata. [14] Kwa nini nijiweke mwenyewe kwenye hatari na kuyaweka maisha yangu mikononi mwangu? [15] Ingawa ataniua, bado nitamtumaini; hakika nitazitetea njia zangu mbele zake. [16] Naam, hili litanigeukia kuwa wokovu wangu, kwa maana hakuna mtu asiyemcha Mungu atakayethubutu kuja mbele yake! [17] Sikilizeni maneno yangu kwa makini; nayo masikio yenu yaingize kile nisemacho. [18] Sasa kwamba nimekwisha kutayarisha mambo yangu, ninajua mimi nitahesabiwa kuwa na haki. [19] Je, kuna yeyote anayeweza kuleta mashtaka dhidi yangu? Kama ndivyo, nitanyamaza kimya na nife. [20] “Ee Mungu, unijalie tu mimi haya mambo mawili, nami sitajificha uso wako: [21] Ondoa mkono wako uwe mbali nami, nawe uache kuniogofya kwa hofu zako kuu. [22] Niite kwenye shauri nami nitajibu, au niache niseme, nawe upate kujibu. [23] Ni makosa na dhambi ngapi nilizotenda? Nionyeshe kosa langu na dhambi yangu. [24] Kwa nini kuuficha uso wako na kunihesabu mimi kuwa adui yako? [25] Je, utaliadhibu jani lipeperushwalo na upepo? Je, utayasaka makapi makavu? [26] Kwa kuwa unaandika mambo machungu dhidi yangu na kunifanya nizirithi dhambi za ujana wangu. [27] Umeifunga miguu yangu kwenye pingu. Unazichunga kwa makini njia zangu zote kwa kutia alama kwenye nyayo za miguu yangu. [28] “Hivyo mwanadamu huangamia kama kitu kilichooza, kama vazi lililoliwa na nondo.