[1] Ndipo Ayubu akajibu: [2] “Bila shaka ninyi ndio watu, nayo hekima itakoma mtakapokufa! [3] Lakini mimi ninao ufahamu kama ninyi; mimi si duni kwenu. Ni nani asiyejua mambo haya yote? [4] “Nimekuwa mtu wa kuchekwa na rafiki zangu, ingawa nilimwita Mungu naye akanijibu: mimi ni mtu wa kuchekwa tu, ingawa ni mwadilifu na nisiye na hatia! [5] Wanadamu wakiwa katika utulivu huwa na dharau kwa wale wenye msiba kana kwamba ndiyo haki ya wale ambao miguu yao inateleza. [6] Hema za wanyangʼanyi hazisumbuliwi, wale wanaomghadhibisha Mungu wako salama: wale wamchukuao mungu wao mikononi mwao. [7] “Lakini ulizeni wanyama, nao watawafundisha, au ndege wa angani, nao watawaambia; [8] au zungumzeni na dunia, nayo itawafundisha, au acheni samaki wa baharini wawape taarifa. [9] Ni nani miongoni mwa hawa wote asiyejua kwamba mkono wa BWANA ndio uliofanya hili? [10] Mkononi mwake kuna uhai wa kila kiumbe, na pumzi ya wanadamu wote. [11] Je, sikio haliyajaribu maneno kama vile ulimi uonjavyo chakula? [12] Je, hekima haipatikani katikati ya wazee? Je, maisha marefu hayaleti ufahamu? [13] “Hekima na nguvu ni vya Mungu; shauri na ufahamu ni vyake yeye. [14] Kile anachokibomoa hakiwezi kujengeka tena; mtu aliyefungiwa naye hawezi kufunguliwa. [15] Akizuia maji, huwa pana ukame; akiyaachia maji, huharibu nchi. [16] Kwake kuna nguvu na ushindi; adanganywaye na adanganyaye, wote wawili ni wake. [17] Yeye huwaondoa washauri wakiwa wametekwa nyara, naye huwapumbaza wanaotoa maamuzi. [18] Huondoa pingu zilizofungwa na wafalme, na kuwafunga mishipi ya kiunoni. [19] Huwaondoa makuhani wakiwa wametekwa nyara, na kuwaangusha waliojiimarisha muda mrefu. [20] Hunyamazisha midomo ya washauri wanaoaminika, na kuondoa busara ya wazee. [21] Huwamwagia dharau wanaoheshimika, na kuwavua silaha wenye nguvu. [22] Hufunua mambo ya ndani ya gizani, na kuyaleta nuruni yale yaliyositirika sana. [23] Huyafanya mataifa yatukuke na kuyaangamiza; hufanya mataifa kuwa makubwa, naye huyatawanya. [24] Huwaondolea viongozi wa nchi akili zao; huwapeleka watangetange nyikani pasipo na njia. [25] Hupapasa gizani pasipokuwa na mwanga; huwafanya wapepesuke kama walevi.