[1] Ndipo Sofari Mnaamathi akajibu: [2] “Je, maneno haya yote yapite bila kujibiwa? Je, huyu mnenaji athibitishwe kuwa na haki? [3] Je, maneno yako ya upuzi yawafanye watu wanyamaze kimya? Je, mtu asikukemee unapofanya dhihaka? [4] Unamwambia Mungu, ‘Imani yangu ni kamili nami ni safi mbele zako.’ [5] Aha! Laiti kwamba Mungu angesema, kwamba angefungua midomo yake dhidi yako, [6] naye akufunulie siri za hekima, kwa kuwa hekima ya kweli ina pande mbili. Ujue hili: Mungu amesahau hata baadhi ya dhambi zako. [7] “Je, waweza kujua siri za Mungu? Je, waweza kuyachunguza mambo yote kumhusu Mwenyezi? [8] Ni juu mno kuliko mbingu: waweza kufanya nini? Kina chake ni kirefu kuliko kuzimu: wewe waweza kujua nini? [9] Kipimo chake ni kirefu kuliko dunia, nacho ni kipana kuliko bahari. [10] “Kama akija na kukufunga gerezani, na kuitisha mahakama, ni nani awezaye kumpinga? [11] Hakika anawatambua watu wadanganyifu; naye aonapo uovu, je, haangalii? [12] Mpumbavu aweza kuwa mwenye hekima, endapo mtoto wa punda-mwitu atazaliwa mwanadamu. [13] “Hata sasa ukiutoa moyo wako kwake na kumwinulia mikono yako, [14] ukiiondolea mbali ile dhambi iliyo mkononi mwako wala usiuruhusu uovu ukae hemani mwako, [15] ndipo utainua uso wako bila aibu; utasimama imara bila hofu. [16] Hakika utaisahau taabu yako, utaikumbuka tu kama maji yaliyokwisha kupita. [17] Maisha yako yatangʼaa kuliko adhuhuri, nalo giza litakuwa kama alfajiri. [18] Utakuwa salama, kwa kuwa lipo tumaini; utatazama pande zote na kupumzika kwa salama. [19] Utalala, wala hakuna atakayekuogofya, naam, wengi watajipendekeza kwako. [20] Bali macho ya waovu hayataona, wokovu utawaepuka; tarajio lao litakuwa ni hangaiko la mtu anayekata roho.”