[1] Mwimbieni kwa furaha, Mungu aliye nguvu yetu; mpigieni kelele za shangwe Mungu wa Yakobo! [2] Anzeni wimbo, pigeni matari, pigeni kinubi na zeze kwa sauti nzuri. [3] Pigeni baragumu za pembe za kondoo dume wakati wa Mwandamo wa Mwezi, na wakati wa mwezi mpevu, katika siku ya Sikukuu yetu; [4] hii ni amri kwa Israeli, agizo la Mungu wa Yakobo. [5] Aliiweka iwe kama sheria kwa Yosefu alipotoka dhidi ya Misri, huko tulikosikia lugha ambayo hatukuielewa. [6] Asema, “Nimeondoa mzigo mabegani mwao; mikono yao iliwekwa huru kutoka kwenye kikapu. [7] Katika shida yako uliniita nami nikakuokoa, nilikujibu katika mawingu yenye ngurumo; nilikujaribu katika maji ya Meriba. [8] “Enyi watu wangu, sikieni, nami nitawaonya: laiti kama mngenisikiliza, ee Israeli! [9] Hamtakuwa na mungu mgeni miongoni mwenu; msimsujudie mungu wa kigeni. [10] Mimi ni BWANA Mungu wako, niliyekutoa nchi ya Misri. Panua sana kinywa chako nami nitakijaza. [11] “Lakini watu wangu hawakutaka kunisikiliza; Israeli hakutaka kunitii. [12] Basi niliwaacha katika ukaidi wa mioyo yao wafuate mashauri yao wenyewe. [13] “Laiti kama watu wangu wangalinisikiliza, kama Israeli wangalifuata njia zangu, [14] ningaliwatiisha adui zao kwa haraka, na kuugeuza mkono wangu dhidi ya watesi wao! [15] Wale wanaomchukia BWANA wangalinyenyekea mbele zake, na adhabu yao ingedumu milele. [16] Bali ninyi mngalilishwa ngano iliyo bora, na kuwatosheleza kwa asali itokayo kwenye mwamba.”