[1] Ee Mchungaji wa Israeli tusikie, wewe umwongozaye Yosefu kama kundi; wewe uketiye katika kiti cha enzi katikati ya makerubi, angaza [2] mbele ya Efraimu, Benyamini na Manase. Uamshe nguvu zako, uje utuokoe. [3] Ee Mungu, uturejeshe, utuangazie uso wako, ili tuweze kuokolewa. [4] Ee BWANA Mungu Mwenye Nguvu Zote, hata lini hasira yako itawaka na kufoka moshi dhidi ya maombi ya watu wako? [5] Umewalisha kwa mkate wa machozi, umewafanya wanywe machozi bakuli tele. [6] Tumekuwa chanzo cha ugomvi kwa jirani zetu, na adui zetu wanatudhihaki. [7] Ee Mungu Mwenye Nguvu Zote, uturejeshe; utuangazie uso wako, nasi tuweze kuokolewa. [8] Ulileta mzabibu kutoka Misri, ukawafukuza mataifa, ukaupanda. [9] Uliandaa shamba kwa ajili yake, mizizi ikawa imara, ukajaza nchi. [10] Milima ilifunikwa kwa kivuli chake, matawi yake yakafunika mierezi mikubwa. [11] Matawi yake yalienea mpaka Baharini, machipukizi yake mpaka kwenye Mto. [12] Mbona umebomoa kuta zake ili wote wapitao karibu wazichume zabibu zake? [13] Nguruwe mwitu wanauharibu na wanyama wa kondeni hujilisha humo. [14] Turudie, Ee Mungu Mwenye Nguvu Zote! Tazama chini kutoka mbinguni na uone! Linda mzabibu huu, [15] mche ulioupanda kwa mkono wako wa kuume, mwana uliyemlea kwa ajili yako mwenyewe. [16] Mzabibu wako umekatwa, umechomwa moto, unapowakemea, watu wako huangamia. [17] Mkono wako na utulie juu ya mtu aliyeko mkono wako wa kuume, mwana wa mtu uliyemlea kwa ajili yako mwenyewe. [18] Ndipo hatutakuacha tena, utuhuishe, nasi tutaliitia jina lako. [19] Ee BWANA Mungu Mwenye Nguvu Zote, uturejeshe; utuangazie uso wako, ili tuweze kuokolewa.