[1] Ee BWANA, Mungu wangu, ninakukimbilia wewe, uniokoe na kunikomboa na wote wanaonifuatia, [2] la sivyo watanirarua kama simba na kunichana vipande vipande, asiwepo wa kuniokoa. [3] Ee BWANA, Mungu wangu, kama nimetenda haya na kuna hatia mikononi mwangu, [4] au ikiwa nimemtenda uovu aliye na amani nami, au nimemnyangʼanya adui yangu pasipo sababu, [5] basi adui anifuatie na kunipata, auponde uhai wangu ardhini na kunilaza mavumbini. [6] Amka kwa hasira yako, Ee BWANA, inuka dhidi ya ghadhabu ya adui zangu. Amka, Mungu wangu, uamue haki. [7] Kusanyiko la watu na likuzunguke. Watawale kutoka juu. [8] BWANA na awahukumu kabila za watu. Nihukumu Ee BWANA, kwa kadiri ya haki yangu, kwa kadiri ya uadilifu wangu, Ewe Uliye Juu Sana. [9] Ee Mungu mwenye haki, uchunguzaye mawazo na mioyo, komesha ghasia za waovu na ufanye wenye haki waishi kwa amani. [10] Ngao langu ni Mungu Aliye Juu Sana, awaokoaye wanyofu wa moyo. [11] Mungu ni mwamuzi mwenye haki, Mungu aghadhibikaye kila siku. [12] Kama hakutuhurumia, atanoa upanga wake, ataupinda na kuufunga uzi upinde wake. [13] Ameandaa silaha zake kali, ameweka tayari mishale yake ya moto. [14] Yeye aliye na mimba ya uovu na achukuaye mimba ya ghasia huzaa uongo. [15] Yeye achimbaye shimo na kulifukua hutumbukia katika shimo alilochimba mwenyewe. [16] Ghasia azianzishazo humrudia mwenyewe, ukatili wake humrudia kichwani. [17] Nitamshukuru BWANA kwa ajili ya haki yake, na nitaliimbia sifa jina la BWANA Aliye Juu Sana.