[1] Ee Mungu, wewe ni Mungu wangu, nakutafuta kwa moyo wote; nafsi yangu inakuonea kiu, mwili wangu unakuonea wewe shauku, katika nchi kame na iliyochoka mahali ambapo hapana maji. [2] Nimekuona katika mahali patakatifu na kuuona uwezo wako na utukufu wako. [3] Kwa sababu upendo wako ni bora kuliko uhai, midomo yangu itakuadhimisha. [4] Nitakusifu siku zote za maisha yangu, na kwa jina lako nitainua mikono yangu. [5] Nafsi yangu itatoshelezwa kama kwa wingi wa vyakula; kwa midomo iimbayo kinywa changu kitakusifu wewe. [6] Kitandani mwangu ninakukumbuka wewe, ninawaza juu yako makesha yote ya usiku. [7] Kwa sababu wewe ndiwe msaada wangu, chini ya uvuli wa mbawa zako naimba. [8] Nafsi yangu inaambatana nawe, mkono wako wa kuume hunishika. [9] Wale wanaotafuta uhai wangu wataharibiwa, watakwenda chini kwenye vilindi vya dunia. [10] Watatolewa wafe kwa upanga, nao watakuwa chakula cha mbweha. [11] Bali mfalme atafurahi katika Mungu, wale wote waapao kwa jina la Mungu watamsifu, bali vinywa vya waongo vitanyamazishwa.