[1] Ee BWANA, tegea sikio maneno yangu, uangalie kupiga kite kwangu. [2] Sikiliza kilio changu ili unisaidie, Mfalme wangu na Mungu wangu, kwa maana kwako ninaomba. [3] Asubuhi, unasikia sauti yangu, Ee BWANA; asubuhi naleta haja zangu mbele zako, na kusubiri kwa matumaini. [4] Wewe si Mungu unayefurahia uovu, kwako mtu mwovu hataishi. [5] Wenye kiburi hawawezi kusimama mbele yako, unawachukia wote watendao mabaya. [6] Unawaangamiza wasemao uongo. BWANA huwachukia wamwagao damu na wadanganyifu. [7] Lakini mimi, kwa rehema zako kuu, nitakuja katika nyumba yako, kwa unyenyekevu, nitasujudu kuelekea Hekalu lako takatifu. [8] Niongoze katika haki yako, Ee BWANA, kwa sababu ya adui zangu, nyoosha njia yako mbele yangu. [9] Hakuna neno kinywani mwao linaloweza kuaminika, mioyo yao imejaa maangamizi. Koo lao ni kaburi lililo wazi, kwa ndimi zao, wao hunena udanganyifu. [10] Uwatangaze kuwa wenye hatia, Ee Mungu! Hila zao ziwe anguko lao wenyewe. Wafukuzie mbali kwa sababu ya dhambi zao nyingi, kwa kuwa wamekuasi wewe. [11] Lakini wote wakimbiliao kwako na wafurahi, waimbe kwa shangwe daima. Ueneze ulinzi wako juu yao, ili wale wapendao jina lako wapate kukushangilia. [12] Kwa hakika, Ee BWANA, unawabariki wenye haki, unawazunguka kwa wema wako kama ngao.