[1] Heri mtu yule anayemjali mnyonge, BWANA atamwokoa wakati wa shida. [2] BWANA atamlinda na kuyahifadhi maisha yake, atambariki katika nchi na hatamwacha katika tamaa ya adui zake. [3] BWANA atamtegemeza awapo mgonjwa kitandani, atamwinua kutoka kitandani mwake. [4] Nilisema, “Ee BWANA nihurumie, niponye, maana nimekutenda dhambi wewe.” [5] Adui zangu wanasema kwa hila, “Lini atakufa, na jina lake litokomee kabisa.” [6] Kila anapokuja mtu kunitazama, huzungumza uongo, huku moyo wake hukusanya masingizio; kisha huondoka na kuyasambaza huku na huko. [7] Adui zangu wote hunongʼonezana dhidi yangu, hao huniwazia mabaya sana, wakisema, [8] “Ugonjwa mbaya sana umempata, kamwe hatainuka tena kitandani mwake.” [9] Hata rafiki yangu wa karibu niliyemwamini, yule aliyekula chakula changu ameniinulia kisigino chake. [10] Lakini wewe, Ee BWANA, nihurumie, ukaniinue tena, ili niweze kuwalipiza kisasi. [11] Najua kwamba wapendezwa nami, kwa kuwa adui yangu hanishindi. [12] Katika uadilifu wangu unanitegemeza na kuniweka kwenye uwepo wako milele. [13] Msifuni BWANA, Mungu wa Israeli, tangu milele na hata milele. Amen na Amen.