[1] Nilimngoja BWANA kwa saburi, naye akaniinamia, akasikia kilio changu. [2] Akanipandisha kutoka shimo la uharibifu, kutoka matope na utelezi; akaiweka miguu yangu juu ya mwamba na kunipa mahali imara pa kusimama. [3] Akaweka wimbo mpya kinywani mwangu, wimbo wa sifa kwa Mungu wetu. Wengi wataona na kuogopa na kuweka tumaini lao kwa BWANA. [4] Heri mtu yule amfanyaye BWANA kuwa tumaini lake, asiyewategemea wenye kiburi, wale wenye kugeukia miungu ya uongo. [5] Ee BWANA Mungu wangu, umefanya mambo mengi ya ajabu. Mambo uliyopanga kwa ajili yetu hakuna awezaye kukuhesabia; kama ningesema na kuyaelezea, yangekuwa mengi mno kuyaelezea. [6] Dhabihu na sadaka hukuvitaka, lakini umefungua masikio yangu; sadaka za kuteketezwa na sadaka za dhambi hukuzihitaji. [7] Ndipo niliposema, “Mimi hapa, nimekuja: imeandikwa kunihusu katika kitabu. [8] Ee Mungu wangu, natamani kuyafanya mapenzi yako; sheria yako iko ndani ya moyo wangu.” [9] Nimehubiri haki katika kusanyiko kubwa, sikufunga mdomo wangu, Ee BWANA, kama ujuavyo. [10] Sikuficha haki yako moyoni mwangu; ninasema juu ya uaminifu wako na wokovu wako. Sikuficha upendo wako na kweli yako mbele ya kusanyiko kubwa. [11] Ee BWANA, usizuilie huruma zako, upendo wako na kweli yako daima vinilinde. [12] Kwa maana taabu zisizo na hesabu zimenizunguka, dhambi zangu zimenikamata, hata nisiweze kuona. Zimekuwa nyingi kuliko nywele za kichwa changu, nao moyo unazimia ndani yangu. [13] Ee BWANA, uwe radhi kuniokoa; Ee BWANA, njoo hima unisaidie. [14] Wote wanaotafuta kuuondoa uhai wangu, waaibishwe na kufadhaishwa; wote wanaotamani kuangamizwa kwangu, warudishwe nyuma kwa aibu. [15] Wale waniambiao, “Aha! Aha!” wafadhaishwe na iwe aibu yao. [16] Lakini wote wakutafutao washangilie na kukufurahia, wale wapendao wokovu wako siku zote waseme, “BWANA atukuzwe!” [17] Lakini bado mimi ni maskini na mhitaji; Bwana na anifikirie. Wewe ndiwe msaada wangu na Mwokozi wangu; Ee Mungu wangu, usikawie.